MBARONI KWA KUCHEZA WAKIWA UCHI STAILI YA KIGODORO

WATU wanne wakazi wa eneo la Masasi Mbovu (Masasi ya zamani) mjini Masasi wanashikiliwa na Polisi kwa tuhuma za kucheza uchi, kwa staili inayoitwa Kigodoro kwenye sherehe ya ndoa.
Mkuu wa Polisi wilayani Masasi, Ndagile Makubi  alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa watuhumiwa hao walikamatwa juzi jioni katika eneo la Masasi mbovu watuhumiwa kutokana na kucheza wakiwa watupu kunakokiuka maadili ya Kitanzania.
Alisema walipata taarifa za kuwepo kwa tukio hilo la kiudhalilishaji kutoka kwa wasamaria wema waliokuwepo kwenye sherehe hizo na kwamba Polisi walifika na kufanikiwa kuwatia mbaroni watuhumiwa hao waliokutwa wakiwa wanaendelea kutoa burudani hiyo kwa mamia ya watu waliojitokeza kwenye sherehe hizo wakiwamo watoto.
Makubi aliwataja wanaoshikiliwa na jeshi hilo kuwa ni pamoja na Anna Yohana (25), Jemima Jordan (22), Aziza Chukachuka (20) na mtoto wa miaka 17 (jina linahifadhiwa) wote wakiwa ni wakazi wa mjini Masasi mkoani Mtwara.
Alisema uchunguzi unaendelea na kwamba watakapobainika kuhusika na tukio hilo la udhalilishaji hasa kwa jinsia ya kike watafikishwa mahakamani kwa taratibu zingine za kisheria.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti, Tiba Matwani na Fatuma Hamisi wamepongeza Polisi wilayani Masasi kwa kuanza operesheni hiyo na kwamba vitendo hivyo vinavyofanywa na wanawake wenzao havistahili kuachiwa vikiendelea kwa kuwa vinadhalilisha utu wao.
Aidha, Kamanda Makubi alizungumzia mikakati iliyowekwa na jeshi hilo mjini humo, ikiwa ni pamoja na kuendesha operesheni maalumu kwenye maeneo yote ya burudani na sherehe mbalimbali ili kuwabaini watu wote wanaokwenda kinyume na maadili ya Kitanzania.

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post