Ticker

6/recent/ticker-posts

KIAMA KWA WAZAZI AMBAO WATOTO WAO WANAPATA MIMBA WAKIWA MASHULENI

Image result for WANAFUNZI WAPATA MIMBA SHULENI
SERIKALI mkoa wa Kilimanjaro imeahidi kuwakamata na kuwachukulia hatua za kisheria wazazi na walezi ambao watoto wao watapewa ujauzito huku wao wakishindwa kuonesha juhudi za kuwasaka wahusika.

Mkuu wa Mkoa huo, Said Mecky Sadiki amesema hayo wakati akikagua ujenzi wa madarasa katika shule ya sekondari Mpirani, kata ya Mabogini wilayani Moshi Vijijini ili kuona matatizo yake.
Kauli ya Mkuu wa Mkoa inatokana na taarifa ya Mkuu wa shule hiyo, Ali Mhando kwamba kwa kipindi cha miezi minane sasa jumla ya wanafunzi wanne wamepewa ujauzito na kuacha shule huku mmoja akiwa tayari amejifungua.
A,esema haiwezekani mwanafunzi akapewa ujauzito huku mzazi ama mlezi wake akikaa kimya bila jitihada za kukemea na kuchukua hatua za kisheria kwa wahusika kama njia mojawapo ya kukomesha vitendo hivyo.
Sadiki alisema serikali haiwezi kuvumilia kuona wanafunzi wanakatishwa masomo na baadhi ya watu wenye nia ovu kwani kwa mujibu wa takwimu mkoa huo kwa kipindi cha kuanzia Januari hadi Agosti mwaka huu, wanafunzi 238 wamepewa ujauzito.
Akikagua vyumba vya madarasa pamoja na matundu 12 ya vyoo vilivyogharimu zaidi ya Sh milioni 88, Sadiki alitaka wananchi kuchangia ujenzi wa vyumba vya madarasa na chakula shuleni badala ya mzigo huo kuwaachia wazazi pekee.
Mkuu wa shule hiyo, Mhando amesema wamebaini watuhumiwa wakuu wa kuwapa wanafunzi ujauzito ni waendesha bodaboda na madereva wa daladala. Amesema wanafunzi wa shule hiyo wanatoka katika vijiji vya Mvuleni, Mtakuja na Mabogini ambapo baadhi yao wanatembea umbali wa zaidi ya kilometa 10 kwenda shule na kurudi, jambo ambalo huwapa vichocheo vya kupata lifti za pikipiki na daladala na kuwapa vishawishi vya mahusiano ya kimapenzi.

Post a Comment

0 Comments