Ticker

6/recent/ticker-posts

WAZIRI WA FEDHA NA MPANGO DKT.PHILIP MPANGO AWASILISHA MAPENDEKEZO YA MPANGO WA MAENDELEO WA TAIFA 2017/2018



Na Eleuteri Mangi, MAELEZO, Dodoma

Serikali imeainisha maeneo ya kipaumbele kwa mwaka 2017/2018 kulingana na mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka ujao wa fedha.
 

Waziri wa Fedha na Mpiango Dkt. Philip Mpango amesema hayo leo Bungeni mjini Dodoma alipokuwa akiwasilisha Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2017/2018 na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2017/2018.

Dkt. Mpango amevitaja vipaumbele hivyo kuwa ni pamoja na miradi ya kielelezo ya maendeleo ambayo inayolenga kufanikisha utekelezaji wa Malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 ni pamoja na miradi ya Makaa ya Mawe Mchuchuma, Mchuchuma Liganga, ujenzi wa reli ya kati kutoka Dar es salaam, Tabora hadi Kigoma yenye urefu wa km 1,251 kwa “Standard Gauge” pamoja na matawi yake ya Tabora kupitia Isaka hadi Mwanza yenye urefu wa km 379, Isaka hadi Rusumo km 371, Kaliua kupitia Mapanda hadi Karema km 321, Keza hadi Ruvubu km 36 na Uvinza hadi Kelelema kuelekea Musongati yenye urefu wa km 203.

Miradi mingine ya kielelezo ni uboreshaji wa Shirika la Ndege TAanzania (ATC), ujenzi wa mitambo ya kusindika gesi mkoani Lindi, uanzishwaji wa Kanda Maalum za Kiuchumimkoani Tanga, Bagamoyo, Kigoma, Ruvuma, uanzishwaji wa kituo cha biashara cha Kurasini, kusomesha vijana katika stadi za mafuta na gesi, uhandisi na huduma za afya.

Waziri Dkt. Mpango ameyataja maeneo mengine ya kipaumbele kuwa ni viwanda vya kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa kukuza uchumi wa viwanda, kufungamanisha maendeleo y uchumi na maendeleo ya watu, mazingira ya wezeshi kwa uendeshaji biashara na uwekezaji, ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi pamoja na maeneo mengine muhimu kwa ukuaji wa uchumi na ustawi wa taifa.

Dkt. Mpango amesema kuwa shabaha ya uandaaji wa mpango wa bajeti ya mwaka 2017/18 unaongozwa Serikali kusimamia mambo ya uchumi kwa ujumla ikiwemo kuongeza kasi ya ukuaji wa pato halisi la taifa kufikia asilimia 7.5 kwa mwaka 2017, asilimia 7.9 mwaka 2018 na asilimia 8.2 mwaka 2019, kudhibiti kasi ya mfumuko wa bei na kuhakikisha kuwa unabaki kwenye wigo wa tarakimu moja kufikia asilimia 5.0 katika kipindi cha muda wakati, kuwa na pato ghafi la taifa la sh. trilioni 123.9 kwa mwaka 2017/18, sh. trilioni 139.7 kwa mwaka 2018/19 na sh. trilioni 165.4 mwaka 2019/20 pamoja na mapato ya kodi kufikia asilimia 14.6 ya pato la taifa mwaka 2017/18, asilimia 15.5 mwaka 2018/19 na asilimia 15.8 mwaka 2019/20.

Aidha, ametaja misingi ya mpango na bajeti kuwa ni amani, usalama, utulivu na utangamano wa ndani ya nchi na nchi jirani ambavyo vitaendelea kudumishwa nchini. Kuhusu mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka 2017/2018, Dkt. Mpango amesema amewaagiza Maafisa Masuuli kuzingatia masuala muhimu wakati wa uandaaji wa mipango na bajeti za mafungu yao ili kutekeleza Sheria ya Bajeti Na. 11 ya mwaka 2015.

Zaidi ya hayo, Dkt. Mpango amesisitiza uwepo usimamizi na udhibiti wa matumizi, ulipaji na ongezeko la madeni ya Serikali, ukusanyaji wa mapato pamoja na mfumo wa utoaji taarifa za utekelezaji.Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti Hawa Ghasia alipokuwa akitoa taarifa ya kamati yake amesema kuwa Kamati yake inardhishwa na hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kusimamia Sheria ya Bajeti na kanuni zake ambayo inahakikisha usimamizi na uwajibikaji katika hatua zote za mchakato wa bajeti unazingatiwa.

Naye Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni Halima Mdee alipokuwa akiwasilisha hotuba yake amesema kuwa Kambi Rasmi inaunga mkono hatua za kisheria zinazochukuliwa na Serikali kwa wale wote waliohusika kwa namna moja au nyingine kuhujumu uchumi wa nchi.

Mkutano wa Tano wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania uanatarajiwa kuhitimishwa Novemba 11 mwaka huu huku shughuli mbalimbali za kuishauri Serikali zikiwasilishwa kupitia mijadala ya Wabunge.

Post a Comment

0 Comments