Mbunge wa jimbo la Arusha mjini Godbless Lema akiwa amezingira na Askari wakimsindikiza kupanda gari la magereza tayari kwa kurudishwa katika mahabusu ya magereza iliopo jijini Hapa
Lema aliyevaa nyeusi akiwa anapanda ndani ya gari
Na Woinde Shizza,Arusha
MBUNGE wa Arusha Mjini, Godbless Lema (Chadema), jana alishindwa
kupata dhamana baada ya mawakili wa Serikali kuwasilisha kwa njia ya
mdomo kusudio la kukata rufaa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha ya kupinga
uamuzi wa dhamana uliotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha jana.
Mawakili hao walisajili kusudio hilo la kukata rufaa, wakiliwasilisha
kwa niaba ya Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP) jana, katika Mahakama
ya Hakimu Mkazi Arusha, mbele ya Hakimu Desderi Kamugisha, baada ya
mahakama hiyo kutupilia mbali maombi ya mawakili hao wa Serikali
walioiomba mahakama hiyo isimpe Lema dhamana.
Akitoa uamuzi huo, Hakimu Desderi alisema baada ya kupitia vipengele
vya Sheria, huku akirejea maamuzi mbalimbali ya Mahakama Kuu kuhusiana
na hoja hiyo, alisema notisi ya kusudio la kukata rufaa inasimama kama
rufaa, hivyo inazuia kutekelezeka kwa maamuzi yaliyotolewa katika
Mahakama hiyo.
Awali akiwasilisha hoja hiyo ya kusudio la kukata rufaa, Wakili
Mwandamizi wa Serikali, Paul Kadushi, alidai mahakamani hapo kuwa wana
kusudio la kukata rufaa na kuwa wameshasajili Mahakama Kuu, hivyo uamuzi
wa Lema kupewa dhamana hauwezi kutekelezeka, kwani umeshapingwa
Mahakama ya juu.
Kwa upande wao, Mawakili wa Utetezi, wakiongozwa na Wakili Charles
Adiel, walidai hawajapata notisi yoyote na kuwa maombi hayo ya kukata
rufaa ni sarakasi za kisheria ambayo yamelenga kuzuia utekelezaji wa
maamuzi yaliyotolewa mahakamani hapo.
Lema alipandishwa katika Mahakama hiyo Novemba 8, akikabiliwa na kesi
mbili za uchochezi, ambapo alishindwa kupata dhamana kufuatia maombi ya
mawakili hao wa Serikali ambao walidai kuwa, Lema anakabiliwa na kesi
nyingine mbili za uchochezi katika mahakama hiyo, asipewe dhamana kwa
kuwa alipopewa dhamana kwa kesi hizo bado alirudia kufanya makosa kama
hayo.
Sababu ya pili ya kuomba mahakama isitoe dhamana hiyo ni kwa ajili ya
usalama wa mshitakiwa, huku sababu ya mwisho ikiwa ni kwa ajili ya
maslahi ya umma.
Akitoa uamuzi huo kuanzia saa 7:02 mchana hadi saa 8:32 mchana,
Hakimu Kamugisha alisema baada ya kupitia hoja za pande zote mbili za
mahakama hiyo, pingamizi la dhamana halikuwa na sababu za msingi, hivyo
mahakama hiyo inatupilia mbali pingamizi hilo na kumpatia mshitakiwa
dhamana ambayo masharti yake yatapangwa na mahakama.
Miongoni mwa sababu za kutupilia mbali pingamizi hilo zilikuwa ni
kuwa mahakama inatoa dhamana bila upendeleo, kwani ni haki ya mshitakiwa
ambayo misingi yake inatajwa katika Ibara mbalimbali katika Katiba ya
Nchi, ikiwa ni pamoja na Ibara ya 16(6) b, ibara ya 15 na ibara ya 17.
Aliieleza mahakama hiyo kuwa, hakubaliani na hoja za upande wa
mashitaka, kwani zinakosa mashiko katika hoja ya kuwa Lema asipewe
dhamana kwa sababu za usalama wake, kwa madai ya kuwa aliyasema maneno
hayo ya uchochezi dhidi ya Rais huku akiwa na bastola ambayo anamiliki
isivyo halali.
Kufuatia malumbano hayo kuhusiana na notisi ya kusudio la serikali
kukata rufaa, kesi hiyo ilikwisha majira ya Saa 10:10 jioni, ambapo
ulinzi mkali uliimarishwa katika eneo la Mahakama hiyo, huku baadhi ya
wafuasi na viongozi wa Chadema, akiwemo Naibu Katibu Mkuu Zanzibar,
Salum Mwalimu, wakizuiwa kuingia katika lango kuu la Mahakama hiyo
ambapo baadaye waliruhusiwa.
Katika kesi ya kwanza Jinai namba 440, Lema anadaiwa kutoa maneno ya
uchochezi Oktoba 22, Mwaka huu, maeneo ya Kambi ya Fisi, Kata ya
Ngarenaro, katika mkutano wa hadhara, alitoa
maneno yenye kuleta tabaka miongoni mwa jamii.
Wakili Marandu alinukuu maneno yanayodaiwa kusemwa na Lema kuwa: “Rais
Magufuli akiendelea na tabia ya kudhalilisha demokrasia na uongozi wa
upinzani, iko siku taifa litaingia kwenye umwagaji wa damu,…. “Rais
yeyote ambaye haheshimu mipaka ya sheria, mipaka ya Katiba, Rais huyo
ataingiza taifa katika majanga na umwagaji damu, watu watajaa
vifua, wakiamua kulipuka polisi hawa wala jeshi halitaweza kudhibiti uhalifu utakaojitokeza.”
Katika kesi ya pili ya Jinai namba 441, Lema anakabiliwa na shitaka la uchochezi, ambapo
anadaiwa kutoa matamshi yenye chuki, kuibua nia ovu kwa jamii.
Alidai kuwa Oktoba 23, mwaka huu, katika mkutano wa hadhara viwanja
vya Shule ya Sekondari Baraa, Lema alitoa maneno kuwa; “Kiburi cha Rais
kisipojirekebisha, Rais akiendelea kujiona yeye ni Mungu, mwaka 2020
haitafika Mungu atakuwa ameshachukua maisha yake.”
Aliendelea kudai kwamba, mtuhumiwa huyo alitoa kauli hizo kinyume cha
Sheria na kifungu cha 63(B) cha kanuni ya adhabu sura ya 16, kama
ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia