Ticker

6/recent/ticker-posts

WATAKIWA KUONGEZA USHIRIKIANO KATIKA MASUALA YA KIJAMII ILI WAPATE TAARIFA


Wakuu wa vituo vidogo, Wakaguzi wa Tarafa pamoja na Polisi kata wameambiwa kwamba wanatakiwa kuwa karibu na wananchi hasa kwa kushiriki shughuli za kijamii kama vile misiba na matatizo mbalimbali hali ambayo itasaidia kupata taarifa nyingi za uhalifu.

Akizungumza katika kikao hicho kilichowahusisha pia watendaji wa kata mbalimbali za halmashauri ya jiji la Arusha kilichofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa bwalo la Polisi lililopo mjini hapa, kamanda wa polisi mkoa wa Arusha Naibu Kamishna (DCP) Charles Mkumbo alisema kutatua matatizo ya kihalifu yanayowakabili wananchi si njia pekee ya kuwa karibu na wananchi bali pia askari hao wanatakiwa kushiriki kwa namna moja au nyingine katika shughuli za kijamii katika maeneo yao.

Alisema kitendo hicho cha askari hao kuishi vizuri na wananchi nje ya kazi yao ya Upolisi kitasabaisha wananchi wajione wapo karibu na askari kwa kila jambo hali ambayo itasaidia kupata taarifa zaidi za kihalifu ambazo hatimaye watazifanyia kazi.
”Ushirikiano wenu pia ujikite kushiriki katika masuala ya kijamii kama vile misiba, lakini pia kuna matatizo mengine kama ya kukatika kwa umeme Polisi kata unapaswa uwasiliane na Tanesco ili kujua tatizo lipo wapi na kisha kuwajulisha wananchi wa kata yako”. Alisema Kamanda Mkumbo.

Aidha Kamanda Mkumbo alisisitiza kudumishwa kwa ushirikiano baina ya askari hao na viongozi wa mitaa pamoja na kata ili kujenga umoja imara utakaosaidia katika kupambana na uhalifu na kuwaeleza watendaji nao wanatakiwa kuwaambia mabalozi wawe na madaftari la usajili wa wageni katika maeneo yao yatayowawezesha kujua tarehe ya kuingia na kuondoka hali ambayo itasaidia kuimarisha usalama.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji wa kata ya Ngarenaro Bw. Brayson Nassari aliendelea kuhimiza ushirikiano katika utendaji wa kazi baina ya Polisi kata na watendaji hali ambayo itasaidia kuimarisha utulivu na amani ndani ya jiji la Arusha.
Naye Mkuu wa Polisi wilaya ya Arusha Mrakibu Mwandamizi (SSP) Emmanuel Tille alizidi kuwasisitiza Polisi kata wawe na vikao vya mara kwa mara na wananchi hali itakayowasaidia kutoa elimu ya ulinzi shirikishi na kupata taarifa lakini pia aliwaeleza watendaji wa kata waendelee kutoa taarifa na kufichua sehemu zenye viashiria vya uhalifu ili zifanyiwe kazi kwa haraka.

Kuwepo kwa mahusiano ya karibu baina ya Jeshi la Polisi mkoa wa Arusha na wananchi kumesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza vitendo vya uhalifu ambapo takwimu za hivi karibu zilizotolewa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Naibu Kamishna (DCP) Charles Mkumbo zinaonyesha kwamba kwa kipindi cha miezi sita toka Januari hadi Juni mwaka huu 2017 uhalifu umepungua kwa 24.4% ikilinganishwa na kipindi kama hiki mwaka jana 2016.

Post a Comment

0 Comments