Ticker

6/recent/ticker-posts

SEREKALI KUHAKIKISHA VIJIJI VYOTE NCHINI VINAUMEME


Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema hakuna kijiji nchini kitakachoachwa bila ya kuunganishiwa umeme katika awamu ya tatu ya mradi unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (Rea).

Amesema Serikali imetenga Sh1 trilioni kwa ajili ya kusambaza umeme katika vijiji 8,000 ambavyo bado havijaunganishiwa na nishati hiyo.

Waziri Mkuu amesema hayo   alipozungumza kwa nyakati tofauti na wananchi wilayani Ruangwa.

Amesema hayo katika mikutano aliyoifanya kwenye vijiji vya Chiapi, Nandanga, Mbecha na Luchelegwa, ikiwa ni siku ya pili ya ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani Lindi.

 “Rais John Magufuli anajali wananchi, hivyo ametenga fedha nyingi zitakazotosheleza kusambaza umeme katika vijiji vyote vikiwemo vya Wilaya ya Ruangwa. Gharama za kuunganishiwa umeme huo ni Sh27,000 tu,” amesema katika taarifa iliyotolewa na ofisi yake.

Amesema wananchi hawatawajibika kulipia nguzo na fomu za maombi ya kuunganishiwa umeme, kwa sababu tayari gharama hizo zimebebwa na Serikali.

Amesema lengo la Serikali ni kufikisha umeme kwenye vijiji vyote Tanzania na kwa vile ambavyo viko kwenye maeneo yaliyo mbali na gridi ya Taifa, vitafungiwa umeme jua (sola) hivyo kufungua fursa za ajira na kukuza uchumi.

Waziri Mkuu amesema huduma hiyo ni muhimu kwa kuwa mbali ya kutumiwa majumbani lakini pia kwa kusogezwa karibu na maeneo ya pembezoni itawezesha zahanati, shule, viwanda na vituo vya afya kuwa na umeme.

Meneja wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) Mkoa wa Lindi, Johnson Mwigune amesema hadi kufikia mwishoni mwa mwezi huu mkandarasi aliyepangwa kufanya kazi katika vijiji hivyo atakuwa ameanza kusambaza umeme.

Post a Comment

0 Comments