Ticker

6/recent/ticker-posts

KABILA LA HADZABE WAPEWA HATI ZA KUMILIKI ARDHI




Na Kitengo cha Mawasiliano - Wizara ya Ardhi

Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi amewapatia hati miliki za Ardhi kwa jamii ya wa Hadzabe wanaoishi wilayani Karatu Mkoani Arusha.

Waziri Lukuvi amefika katika maeneo yao na kuwapa hati miliki za kimila kwa vijiji na wanayoishi jamii ya wa Hadzabe na jamii nyingine za kifugaji ili kulinda maeneo yao ya malisho na maeneo wanayotumia kuwinda wanyama.

Jamii ya wa Hadzabe ni watu ambao huishi kwa mfumo wa maisha ya kuwinda, kufuga wanyama pori na kula mimea na matunda ya miti inayowazunguka. Jamii hii kwa miaka mingi imekuwa ikiishi bila kufuata mipaka ya maeneo yao na hivyo kusababisha migogoro ya ardhi kwa jamii nyingine zinazoishi karibu na maeneo yao.

Pamoja na ziara hiyo Mhe. William Lukuvi amtatua migogoro ya Ardhi ya wananchi wa wilayani Karatu Mkoani Arusha na wananchi walio na kero za migogoro ya ardhi na kuzipatia ufumbuzi pamoja na kupokea vielelezo vya kero za wananchi walizoziwasilisha kwa Waziri ili azitolee maamuzi.

Wananchi wa vijiji vya Mang’ola juu na Midabini wilayani Karatu Mkoani Arusha walisimamisha msafara wa Mhe. Lukuvi ili awasikilize kero zao za ardhi, ambapo Waziri Lukuvi alisimama na kuzitatua pamoja na kumuagiza Mkuu wa wilaya ya karatu Bibi Therezia Mahongo kutafutia ufumbuzi baadhi ya migogoro hiyo.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi anaendelea na Ziara zake za utatuzi wa Migogoro ya Ardhi nchini, ambayo imejikita zaidi katika kutatua migogoro ya ardhi ya Mikoa ya kanda ya Magharibi, Kaskazini na ile ya Kanda ya Ziwa hapa nchini.

Hadi sasa Mhe. Lukuvi ndani ya mwezi huu wa Desemba ameishatatua migogoro ya ardhi ya Mkoa wa Kigoma na wilaya zake za Kigoma mjini, Kasulu na Kibondo na katika Mkoa wa Shinyanga na wilaya zake za Kishapu na Shinyanga mjini na katika mkoa wa Geita amefanya ziara katika wilayani Chato.

Pia Mhe. Lukuvi ametatua migogoro ya ardhi ya Mkoa wa Mara katika wilaya za Musoma na Bunda ambapo kwa Arusha ametatua migogoro ya wilaya ya Arumeru na Karatu.

Post a Comment

0 Comments