Ticker

6/recent/ticker-posts

BONDIA SWALEH MASUDI APIGWA MERERANI

Bingwa wa ngumi wa uzito wa kilo 68 wa Mkoa wa Manyara, Ramadhan Songe kutoka wilaya ya Simanjiro, ametetea ubingwa wake kwa kumpiga bondia wa Mji mdogo wa Mirerani, Swaleh Masudi.
 
Songe alishinda pambano hilo la raundi 10 juzi Kazamoyo Inn, lililoandaliwa na Kampuni ya Ken Family, kupitia Nick Electronics, Pub and Barber shop ya Mji mdogo wa Mirerani, chini ya Mkurugenzi wake Kilonzo Kalaghe.
 
Akizungumza na waandishi wa habari, Meneja wa Ken Family, Ally Kayoyo alisema Songe alishinda pambano hilo lililosimamiwa na Mwenyekiti wa CCM wa kata ya Endiamtu Issa Katuga, kwa kupata alama 50 kwa 20.
 
“Kupitia Mkurugenzi wetu Kilonzo Kalaghe tumeamua kudhamini ngumi na tutaendelea kuleta mapambano mengine kwa ajili ya kunyanyua michezo katika maeneo ya mji mdogo wa Mirerani na Manyara kwa jumla,” alisema Kayoyo.
 
Hata hivyo, akizungumza baada ya kumalizika pambano hilo na kutangazwa mshindi, Songe alisema anastaafu kucheza ngumi kwani hivi sasa hana mpinzani kwenye mkoa huo, hivyo anatumia muda wake kwa kuwafunda vijana chipukizi.
 
“Kwa vile ngumi zipo kwenye damu yangu nitawafundisha vijana wenye nia ya kujifunza ndondi, ili kuuendeleza mchezo huu ambao nimetumia nguvu zangu nyingi kwa ajili ya kuunyanyua katika mkoa wa Manyara,” alisema Songe.  
 

Post a Comment

0 Comments