Ticker

6/recent/ticker-posts

VITUO VYA AFYA VYA VIJIJINI MKOANI MANYARA NJIANI KUFUNGIWA UMEME



Vituo sita vya afya vilivyopo Wilaya ya Babati na Hanang’ Mkoani Manyara, ambavyo vilikuwa vinatoa huduma ya afya vijijini bila nishati ya umeme tangu vianzishwe, vitafungiwa nishati hiyo ili viondokane na tatizo hilo.
 
Akizungumza na waandishi wa habari juzi mjini, Mkurugenzi wa kampuni ya Lucas-EMS, Mhandishi Samwel Kessy alisema kampuni yake imejiandaa ipasavo kuhakikisha vituo hivyo vya afya vinanufaika ipasavyo na nishati hiyo.
 
Mhandisi Kessy alitaja vituo hivyo vya afya ambavyo vimeshafungiwa nishati hiyo ya umeme hafi hivi sasa ni Qameyu na Secheda vilivyopo wilayani Babati na kituo cha afya cha Bassodesh kilichopo wilayani Hanang.
 
Alisema katika mpango huo wanatarajia kufunga nishati ya umeme wa jua na upepo ambapo hivi sasa vituo hivyo vitatu vimeshanufaika na huduma hiyo na vituo vya Gidas cha Babati, Dumbeta na Getanuwas vya Hanang’ vitafuata.
 
“Mfumo huo wa umeme ambao unatumia nguvu ya upepo na mionzi ya jua kwa pamoja, utafanya kazi kwenye jokofu la kuhifadhi dawa, taa, kompyuta, kipimo cha damu, radio, runinga, X ray na vinginevyo,” alisema Mhandisi Kessy.
 
Nao, baadhi ya wauguzi wa vituo hivyo vya afya, Paulina Tsaxara, Adelina Munishi na Juliana Nyalolo, wamepongeza hatua hiyo ya kuwekewa umeme kwani awali walikuwa wanatoa huduma kwa jamii katika mazingira magumu.  
 
Walisema hivi sasa huduma zao zitakuwa makini baada ya kufungiwa nishati hiyo ya umeme ambayo awali ilikuwa vigumu kufanya shughuli zozote zinazohitaji umeme hivyo kuwakwamisha kwa kiasi kikubwa.

Post a Comment

0 Comments