Ticker

6/recent/ticker-posts

HIVI VIVYO JINSI LOWASSA ANAVYOITESA CCM! NI SHIDA

HOFU ya harakati za Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, kuwania urais katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwakani imezidi kukitesa Chama Cha Mapinduzi (CCM), safari hii Umoja wa Vijana wa chama hicho (UVCCM), ukitaka atimuliwe.

Jana UVCCM imemtaka Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Philip Mangula, kuwang’oa watu wanaotangaza kuwania uongozi kabla ya wakati, na wanaomwaga fedha kwa wajumbe wa mkutano mkuu ili kuwashawishi wawaunge mkono katika nia zao.

Tamko hilo la UVCCM linakazia kauli iliyotolewa wiki iliyopita na Mangula, kuwa CCM itawaadhibu makada wake wanaotangaza au kufanya kampeni za urais kabla ya wakati uliowekwa na chama hicho.
Wakati chama hicho kikionekana kutikiswa na ushawishi wa Lowassa, mbunge huyo anadaiwa kuendelea kujiimarisha katika kile alichokiita safari ya kuwapatia Watanzania elimu bure kwa kukutana na wafanyabiashara wa mkoani Arusha.

Tanzania Daima Jumapili, limedokezwa kuwa Januari 2, mwaka huu, Lowassa aliendelea na harakati zake za kujipanga kugombea urais 2015 kwa kuwaandalia chakula cha mchana marafiki zake zaidi ya 100.
Hafla hiyo ilifanyika majira ya saa saba mchana kwenye eneo la Papa King lililopo karibu na hoteli ya Lush Garden ambalo hutumika kwa michezo ya watoto.
 

Kwenye hafla hiyo, Lowassa hakutoa hotuba, badala yake alikuwa anapita kwenye meza za wageni wake na kuwashukuru kwa kuhudhuria ibada yake ya shukurani aliyoifanya siku ya mwaka mpya.Kwa mujibu wa mmoja wa watu walioshiriki kwenye hafla hiyo, mbunge huyo alikuwa akiwaomba wasisite kuitikia wito wake wa kukutana nao Juni 1, mwaka huu.

Alibainisha kuwa mkutano huo wa Juni 1 utawakutanisha marafiki, wanasiasa na wafanyabiashara mbalimbali, na watachangisha fedha za kutekeleza mikakati yake ya kuifikia safari aliyoianza mwaka huu.
Katika kikao kilichofanyika Januari 2, mwaka huu, kada wa CCM aliyekuwa mbunge katika Mkoa wa Mwanza mwaka 2005-2010, alikabidhiwa jukumu la kuratibu posho na fedha za kujikimu kwa baadhi ya watu waliohudhuria.

UVCCM wataka atimuliwe
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Katibu Idara ya Uhamasishaji na Chipukizi Taifa, Paul Makonda, alisema Kamati ya Maadili inayoongozwa na Mangula, inapaswa itafasiri hasira ya wanaCCM kwa vitendo.

Makonda alisema UVCCM wameamua kuwa wakali kwa watu wasiofuata kanuni na ilani ya chama chao, ambacho kinaweza kuanguka kama kisipowadhibiti.

Ingawa katika mkutano wa jana Makonda hakutaja majina ya makada wa CCM wanaodaiwa kukiuka kanuni kwa kutangaza nia mapema, lakini anaonekana kumlenga Lowassa.

Licha ya kuonekana kumlenga Lowassa, si Mangula wala Makonda waliokuwa na ubavu wa kutaja hadharani jina la mbunge huyo aliyetangaza safari ya kuwaletea Watanzania elimu bure na huduma bora za kijamii.

Lowassa katika hotuba yake ya kufunga mwaka 2013 na kuukaribisha mwaka mpya 2014 nyumbani kwake Monduli, alikaririwa akisema ameanza rasmi safari aliyoiita ya matumani ya ndoto zake, ambayo pia itatimiza ndoto za Watanzania za kupata elimu bure, maji safi na maendeleo ya uhakika.

Mbunge huyo ambaye amekuwa akitajwa kuwa mmoja wa wagombea wa nafasi ya urais kupitia CCM katika uchaguzi mkuu wa 2015, aliyasema hayo katika ibada ya shukrani ya kuupokea mwaka mpya, katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Monduli.

Katika hafla hiyo, Lowassa anadaiwa kuwasafirisha baadhi ya wajumbe wa vikao muhimu vya uamuzi vya chama na kuwapa fedha, malazi na kadi za Krismasi ambazo zinadaiwa kuambatanishwa na fedha.

Kauli ya UVCCM, kumuonya Lowassa na wengine wanaodaiwa kuvunja kanuni, inafanana na ile ya Katibu wa Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye na ya Mangula, ambaye alikaririwa hivi karibuni kuelezea kuundwa kwa timu ya kuwachunguza makada wake wanaodaiwa kutangaza nia ya kuwania uongozi kabla ya wakati.

Kwa upande wa Nape, yeye alikaririwa akidai kuwa Lowassa amevunja kanuni, hivyo kupoteza sifa ya kugombea nafasi za uongozi ndani na nje ya CCM.

Makonda alisema kuwa vijana wa CCM hawatakubali kuona mshikamano unavunjika kwa sababu ya watu wanaogawa fedha na kuahidi kutoa elimu bora.“Watu wanatangaza kutoa elimu bora kwanini wasifanye hayo kupitia chama, kinachofanywa sasa ni mwelekeo wa kubomoa mshikamano ndani ya CCM, kudhoofisha na hatimaye kutuengua katika uongozi wa nchi,” alisema.

Makonda alisema watu hao ni wasaliti wasio na woga wala aibu kwa kujiaminisha kuwa wanagombea urais, ubunge, udiwani na nafasi nyingine za kupigiwa kura baada ya kuanza kampeni za kishindo za rushwa na vishawishi mbalimbali nje ya utaratibu, kanuni na maadili ya CCM.

“Hali hii inatishia kabisa kutoweka kwa mshikamano ndani ya chama, na inasababisha makundi yanayoundwa na wagombea hawa wasio rasmi yanayopita nchi nzima kushawishi kwa fedha na rushwa nyingine kwa makundi ya kijamii, ya kijasiriamali ili kuungwa mkono.

“Watu hawa wameweka pembeni ilani ya CCM ya 2010 na kutumia ilani zao binafsi za kumwaga pesa nchi nzima, kusambaza elimu kama njugu bila kuelezea vyanzo vya mapato vya serikali zao za kusadikika,” alisema.

Alisema kuwa CCM ina taratibu za kupata uongozi, hivyo kufanya kinyume ni uasi, upungufu wa busara na ukosefu wa sifa ya uongozi hali inayozidi kukitia doa chama.“Dhamira ya CCM ni kutuunganisha wote kuwa kitu kimoja, dalili zozote nje ya tunu hizo ni usaliti, hauna budi kupigwa vita kwa nguvu zote, hasa sisi vijana, na tusiangalie nyani usoni kwani hakuna mtu yeyote aliye juu au mkubwa kuliko chama, hivyo bandu bandu hii iliyoanza tusiivumilie itatuweka pabaya,” alisema Makonda.

Alisema kuwa asiyetaka kufuata maadili, miiko na kanuni za CCM ni ruksa kuondoka.

Post a Comment

0 Comments