Ticker

6/recent/ticker-posts

WAKULIMA WA ZAO LA UFUTA WATAKIWA KUJIUNGA NA MPANGO WA STAKABADHI YA GHALANI

Wakulima wa zao la ufuta wa Tarafa ya Mbugwe, Wilaya ya Babati Mkoani Manyara, wametakiwa kujiunga na mpango wa stakabadhi ghalani ili kunufaika kiuchumi kuliko kunyonywa na walanguzi.
 
Wito huo ulitolewa na Ofisa masoko wa shirika la Farm Africa, Rahel Pazzia wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo wakulima wa zao la ufuta, yaliyofanyika juzi kwenye kijiji cha Mwada wilayani Babati.
 
Pazzia alisema kati ya wakulima 920 wa zao hilo katika eneo la Mbugwe, ni wakulima 135 pekee waliojiunga na mfumo wa stakabadhi ghalani na wakiulizwa kwanini hawajiungi na mfumo hawana jibu sahihi la kutoa.
 
“Mfumo wa stakabadhi ghalani unafaida kwa mkulima kwani unatumia bidhaa zilizohifadhiwa kama dhamana, badala ya mali na kuliko kuweka nyumba au kiwanja rehani ili kupata mkopo na wengi wamekopeshwa,” alisema Pazzia.
 
Naye, Ofisa ushirika wa halmashauri ya mji wa Babati, William Mbogoro, akizungumza kwa niaba ya bodi ya leseni za maghala nchini alisema wadau wa mfumo huo ni mweka mali, mtunza ghala, asasai za fedha, taasisi za Serikali na mnunuzi.
 
Mbogoro alisema mfumo wa stakabadhi ghalani una manufaa kwa wakulima kwani uwezo wao wa kuhifadhi mazao ni mdogo na hawafahamu namna bora ya kuyapanga hivyo kusababisha kupunguza ubora wake.  
 
Nao baadhi ya wakulima hao wa ufuta, Haji Daudi, Katarina Madolo, Mwajuma Lubuva na Philemon Lissu, walidai kuwa watajiunga na mfumo huo kwani awali walikuwa hawajatambua umuhimu wake.
 
Walisema kupitia dhana ya stakabadhi ghalani watayaweka mazao yao sehemu husika na kuwa dhamana ya kupatiwa mikopo kwenye taasisi za fedha kuliko kuweka nyumba, kiwanja au gari hivyo kufilisiwa pindi ukishindwa kurudisha.
 

Post a Comment

0 Comments