Ticker

6/recent/ticker-posts

CAG ACHUNGUZA UFISADI UNAOFANYIKA TPRI

TAASISI ya Utafiti wa Dawa za Mimea na Wadudu (TPRI) yenye makao makuu mkoani Arusha imekumbwa na kashfa ya ubadhirifu wa fedha zaidi ya sh milioni 317 ambazo hazijulikani matumizi yake mpaka sasa.
Kutokana na tuhuma hiyo, Ofisi  ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) imetuma tume ya watu watano kufanya ukaguzi wa ubadhirifu wa fedha hizo zinazodaiwa kuwa na utata wa matumizi yake.
Tume hiyo inayoongozwa na Edmund Gratian inatokana na maagizo yaliyotolewa kwa ofisi hiyo ya CAG na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) chini ya Mwenyekiti wake, Zitto Kabwe, baada ya kubainika kuwepo kwa wasiwasi wa ubadhirifu huo.
Kwa mujibu wa kamati hiyo, wasiwasi huo ulitokana na kiasi hicho cha fedha kutolewa na Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwenda kwa TPRI kwa ajili ya kutekeleza tafiti mbalimbali zinazofanywa na taasisi hiyo na kisha kurejeshwa wizarani bila kuandikiwa ripoti wala maelezo yoyote.
Mbali na ubadhirifu huo, tume hiyo inachunguza pia kuwepo kwa mazingira tata ya uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo, Epiphania Kimaro, kwa kuwa yaligubikwa na mizengwe na mazingira ya rushwa na hayakufuata mfumo sahihi.
Zitto alisema kabla ya uteuzi huo Bodi ya TPRI iliteua majina matatu ya watumishi waliokuwa na sifa ya kushika nafasi hiyo na kuwasilisha wizarani, lakini cha kushangaza baadaye aliteuliwa mtu tofauti kushika nafasi hiyo, tena asiye na sifa na kuahidi kuwa kamati yake itafuatilia kujua sababu za maoni ya bodi kutofuatwa katika uteuzi huo.
Wakizungumza na waandishi wa habari baadhi ya wafanyakazi wa taasisi hiyo walisema wamefurahishwa na hatua ya serikali kuleta tume hiyo kufanya uchunguzi, kwakuwa itabaini mengine mengi.
Walisema Machi mwaka jana wafanyakazi saba wakiwamo wanne wa Idara ya Uhasibu na watatu wa idara nyingine walifukuzwa kazi kutokana na ubadhirifu wa zaidi ya sh milioni 360 wa fedha za mishahara.

Post a Comment

0 Comments