Tanzania itapata nini kwa kuihujumu Rwanda?

 
Serikali mwishoni mwa wiki ililazimika kukanusha vikali habari iliyochapishwa na gazeti la Serikali ya Rwanda kwamba Rais Jakaya Kikwete anavisaidia vikundi vya waasi nchini humo kuihujumu Serikali ya Rais Paul Kagame.
Pasipo kuthibitisha au kuonyesha vyanzo vya tuhuma hizo ambazo Serikali ya Tanzania imesema hazina msingi wowote, Gazeti hilo la ‘The News of Rwanda’ limeonyesha wazi kwamba, huenda limebeba ajenda ya siri inayosukumwa na baadhi ya wanasiasa nchini humo ya kuharibu uhusiano kati ya nchi hizo mbili.
Tamko la Serikali kupitia kwa Kaimu Balozi wa Tanzania nchini Rwanda, Francis Mwaipaja limesema Rais Kikwete amesikitishwa na habari hizo za uongo na kusema zinaweza kujenga chuki na kuwachanganya wananchi wa nchi hizo jirani na rafiki.
Jambo ambalo tunadhani Serikali ya Tanzania itahitaji ufafanuzi kutoka Kigali ni msimamo wa Serikali ya Rwanda kuhusu tuhuma hizo zilizochapishwa na gazeti hilo inalolimiliki. Itakuwa vigumu kwa Serikali kujenga hoja kwamba gazeti lake lilichapisha tuhuma hizo nzito pasipo serikali yenyewe kujua na pengine kuridhia.
Tunaposema hivyo hatuna maana kwamba uhusiano kati ya nchi hizo mbili umekuwa imara siku zote.
Mwaka uliopita uhusiano kati ya viongozi wa nchi hizo mbili ulidorora baada ya Rais Kikwete kumshauri Rais Kagame kufanya mazungumzo na vikundi vya waasi vya FDLR na RNC ili kupata maridhiano, lakini Rais huyo aliuchukulia ushauri huo kama matusi kwa nchi yake na kusema hawezi kukaa pamoja na watu aliodai walifanya mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 ambapo watu zaidi ya 800,000 waliuawa.
Vilevile, kitendo cha majeshi ya ulinzi ya Tanzania mwaka jana kushiriki kupambana na kukisambaratisha kikundi kilichokuwa kikihusishwa na Serikali ya Rwanda cha M23, ambacho kilikuwa kikiendesha hujuma dhidi ya Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), kilimkasirisha sana Rais Kagame.
Hali hiyo ilisababisha Kenya, Uganda na Rwanda kuitenga Tanzania katika baadhi ya mambo muhimu katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Hata hivyo, wakati juhudi za kurejesha uhusiano baina ya nchi hizo mbili zikionekana kuzaa matunda, ndipo gazeti hilo lilipoibuka na habari hizo za kutunga dhidi ya Rais Kikwete na serikali yake kwa lengo la kuweka mazingira magumu ili kukwaza juhudi hizo.
Kama tulivyosema hapo juu, wapo watu wanaofaidika inapokuwapo hali ya kutoelewana baina ya viongozi wa nchi hizo jirani na rafiki.
Tunasema hivyo, kwa sababu inawezekanaje gazeti limtuhumu Rais Kikwete kwamba katika nyakati tofauti mjini Dodoma na Ikulu jijini Dar es Salaam alikutana na Waziri Mkuu wa zamani wa Rwanda, Faustine Twagiramungu pamoja na viongozi wa RNC na makamanda wa FDLR, wakati dunia nzima inajua kwamba wakati huo alikuwa Davos, Uswisi akihudhuria Mkutano wa Dunia Kuhusu Uchumi (WEF), ambapo alikutana na viongozi mbalimbali duniani, wakiwamo Naibu Waziri Mkuu wa Uingereza, Niuck Clegg na Mkuu wa USAID, Rajiv Shah.
Tunashangazwa pia na madai ya gazeti hilo eti Tanzania imeanzisha taasisi ya kuwasaidia waasi wa Rwanda na ilitoa pasi za kusafiria kwa viongozi wa makundi ya waasi yaliyotajwa hapo juu. Tunaishauri Serikali kuchunguza chanzo cha tuhuma hizi za kuchonga. Hivi Tanzania itapata nini kwa kuihujumu nchi kama Rwanda?

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia