Trafiki wala rushwa sasa kusota njaa


Kikosi cha Polisi cha Usalama Barabarani nchini, kina mpango wa kuanzisha utaratibu mpya wa kulipa faini zote za makosa ya barabarani kupitia benki na mitandao ya simu za mkononi.
Utaratibu huo unalenga katika kupunguza malalamiko ya wananchi kuhusu vitendo vya rushwa vinavyofanywa na baadhi ya askari wa usalama barabarani.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili, Kamanda wa Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mpinga, alisema utaratibu huo unatarajiwa kuanza wakati wowote ndani ya mwaka huu baada ya makao makuu ya jeshi hilo, kuuidhinisha.
Alisema kwa sasa jeshi hilo lipo katika mchakato wa kuhakikisha kuwa utaratibu huo unaanza mapema.
Alisema chini ya mfumo huo, mlipaji atapewa risiti ya benki au mtandao wa simu ambao malipo hayo yatapitia.
“Muda wowote ndani ya mwaka huu utaratibu mpya utaanza, tunataka kuboresha mfumo wa ulipaji faini na kuondokana na mianya ya rushwa inayofanywa na baadhi ya askari wa usalama wa barabarani kama inavyolalamikiwa na wananchi” alisema Kamanda Mpinga.
Alisema licha ya mfumo huo kuwa mpya viwango vya faini zitakazotozwa havitabadilishwa wala kuongezwa.
Kuhusu askari wa kikosi hicho wenye vitabu bandia vya faini kuwa sababu ya kubadilisha utaratibu wa sasa, Kamanda Mpinga alisema ofisi yake haijapata taarifa za uhakika wala ushahidi kuhusu vitabu hivyo.
“Tatizo hili linazungumzwa hakuna taarifa kamili za kupatikana kwa vitabu feki lakini vitabu hivyo vinaweza kuwepo na vikatumika kinyume na sheria ndiyo maana tutaanzisha utaratibu huu,” alisema kamanda.

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia