Viongozi CCM wazidi kuvurugana urais mwaka 2015


Aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa, amewaonya wanachama wa chama hicho wenye nia ya kugombea nafasi za uongozi katika uchaguzi mkuu ujao akiwataka kuzingatia kanuni za chama hicho, vinginevyo watahukumiwa.
Akizungumza na gazeti hili jana, Msekwa alisema watu hao watahukumiwa na chama akieleza kwamba kutangaza nia kabla ya wakati ni kukiuka kanuni za CCM, zinazoeleza wazi kuwa wagombea wa nafasi mbalimbali, watajitangaza baada ya chama kutoa ratiba yake.
Wakati Msekwa akieleza hayo, Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Sadifa Juma Khamis amesema kuwa kutangaza nia ya kugombea nafasi yoyoye ndani ya chama hicho siyo dhambi.
Naye Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Khamis Mgeja ameshambulia Makamu Mwenyekiti mstaafu wa chama hicho John Malecela aliyetaka CCM imchukulie hatua Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kwa madai ya kuanza mapema kampeni za kusaka urais wa mwaka 2015, hatua inayotafsiriwa kuwa ni kuzidi kuvurugana kwa chama hicho.
Msekwa alisema kuwa CCM inaongozwa kwa mujibu wa kanuni na Katiba yake na kwamba katika jambo hilo linaloibuka sasa, kanuni ndiyo zinazohusika zikielekeza wazi mgombea afanye nini na kwa wakati gani.
“Mimi mwenyewe nilishiriki kuandika kanuni hizo, utakapofika wakati chama kitatoa ratiba yake na kila mwenye nia atakuwa na uhuru wa kueleza nia yake. Lakini kutangaza kugombea sasa kabla ya wakati, ni kukiuka kanuni za CCM na ni kosa kubwa,” alisema Msekwa.
Aliwataka wanaCCM wote kuepuka kukiuka kanuni za chama hicho akisisitiza kuwa wote watakaohusika kuzivunja, wataadhibiwa kwa mujibu wa Kanuni na Katiba ya chama hicho.
Alisema kuwa wanaodhani kwa kufanya hivyo wanakivuruga chama, wanafanya makosa kwani watakaoathirika ni wale wanaovunja kanuni zilizowekwa.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), Sadifa Juma Khamis alionyesha kupingana na maneno hayo ya Msekwa, huku yeye akisema kutangaza nia ya kugombea nafasi yoyote ndani ya chama siyo kosa, mradi mhusika awe na nia, sifa na uwezo.
Alisema kuwa ingawa UVCCM haijakaa kujadili watu hao, lakini haoni kosa lolote kwa mwanaCCM kujitokeza na kutangaza nia yake hadharani.Wakati huo huo, Katibu wa Uhamasishaji na Chipukizi katika Umoja wa Vijana (UVCCM), Paul Makonda ametakiwa kuwaomba radhi viongozi wa dini kutokana na kauli yake ya hivi karibuni kuwa masheikh na maaskofu wakiwemo vijana wanaotaka fedha za bure waende kwa Edward Lowassa.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekliti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Khamisi Mgeja alisema licha ya Makonda kuomba radhi, Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), utoe tamko kueleza iwapo kauli hiyo ni ya Makonda au ndiyo msimamo wa Jumuia. “Nataka mwenyekiti wa UVCCM Taifa kutoa tamko kuhusu kauli hiyo na pia viongozi wa dini waombwe radhi kwani walichofanyiwa ni udhalilishaji,” alisema Mgeja.

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia