MILIONI 20 ZAPATIKANA KWENYE ARAMBEE YA MFUKO WA ELIMU NAISINYAI

ZAIDI ya Sh20 milioni zimepatikana kwenye harambee ya mfuko wa elimu wa kata ya Naisinyai Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara wenye lengo la kulipia gharama za masomo kwa wanafunzi wa sekondari wanaoishi katika mazingira magumu.

Akizungumza kwenye harambee ya mfuko huo iliyofanyika juzi,Diwani wa kata ya Naisinyai,Klempu Ole Kinoka alisema  mfuko huo ulianzishwa Machi 18 mwaka 2010 na hadi sasa umewezesha kuwasomesha watoto 76 wa kata hiyo.

Ole Kinoka alisema mfuko huo utakuwa endelevu kwa kuchangiwa kila mwaka na utawanufaisha wanafunzi wa shule za sekondari za Naisinyai na Ewong’on za kata hiyo wenye uelewa mkubwa darasani lakini wazazi wao wana hali duni.

Alisema kila mkazi wa kata hiyo mwenye umri wa miaka 18 kila mwaka anachangia sh10,000 kwa lengo la kutunisha mfuko huo wenye kusimamiwa na kamati ya maendeleo ya kata baada ya wananchi kupitia majina ya watoto hao.  

“Jamii itaona manufaa na matunda ya kuchangia mfuko huu baada ya miaka ijayo kwa watoto wetu kwani hili jambo siyo kama mahindi unapanda leo baada ya miezi kadhaa unavuna faida yake itaonekana hapo baadaye,” alisema Ole Kinoka.

Naye,Ofisa Mtendaji wa kata ya Naisinyai,Yeniel Kagonji alisema mfuko huo unakabiliwa na changamoto ya kuongezeka kwa idadi kubwa ya watoto tegemezi na ukame unaoathiri mifugo na kilimo kwa wananchi.

Kagonji alitaja changamoto nyingine ni uelewa mdogo wa baadhi ya jamii juu ya faida ya uchangiaji wa elimu,wazazi kukabiliwa na michango mingi ya elimu kwa asasi za elimu na kupanda kwa bei za vifaa na gharama za elimu kuongezeka.

Alisema kutokana na mafanikio ya kuwasomesha watoto hao 76 jamii nyingi za kata hiyo zimepata moyo na kuhamasika kuchangia michango mingine ya maendeleo na umewaokoa watoto wengi kupunguza utoro na kuongeza ufaulu.

Alisema malengo ya kuanzishwa kwa mfuko huo ni kuunga mkono mchakato wa mpango wa Serikali wa kutekeleza mkakati wa kukuza uchumi na kupunguza umasikini (Mkukuta) na kuwasaidia watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu.

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia