ATAKA WAZIRI WA ZAMANI WA MIPANGO WA RWANDA AACHIWE HURU

Wakili wa utetezi katika kesi inayomkabili Waziri wa zamani wa Mipango , Augustin Ngirabatware Jumatano aliiomba Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) kumwachia huru mteja wake kwa madai kwamba mwendesha mashitaka ameshindwa kuthibitisha mashitaka pasipo mashaka.
 
‘’Ushahidi uliotolewa na Ngirabatware ni zaidi ya ushahidi wa kuaminika na umeonyesha zaidi ya vigezi vya kuwepo  mashaka katika kesi ya mwendesha mashitaka hivyo hamna budi kumwachia huru,’’ Wakili Kiongozi, Mylene Dimitri aliiambia mahakama iliyokuwa inaongozwa na Jaji William Sekule.
 
Dimitri ambaye alikuwa anatoa hoja za mwisho katika kesi ya mteja wake alidai kwamba ushahidi wa Ngirabatware kuwa kamwe hakushiriki katika mauaji dhidi ya Watutsi katika wilaya ya Nyamyumba, mkoa wa Gisenyi, Kaskazini mwa Rwanda alikozaliwa ulikuwa ‘’ wenye maana, haikuegemea upande wowote na wa kuaminika kwa kiwango cha hali ya juu,’’ 
 
Wakati wa usikilizaji wa kesi yake, Ngirabatware alitoa sababu kadhaa kwamba hakuwapo nyumbani kwao wakati uhalifu ulipokuwa unafanyika. Alidai kwamba kati ya Aprili 23 na Mei 23, 1994, alikuwa katika safari za kikazi katika nchi mbalimbali zikiwemo, Senegal, Gabon na Uswisi.
 
Lakini kwa upande wake mwendesha mashitaka alikuwa na maelezo tofauti kuwa katika kipindi hicho, mshitakiwa alikuwa mkoani Gisenyi, hususan ni katika wilaya yake ya Nyamyumba akidaiwa kushiriki katika kutenda uhalifu huo.
 
Kwa mujibu wa wakili huyo, Ngirabatware aliwasilisha nyaraka kadhaa kudhibitisha hoja zake ikiwa ni pamoja na hati yake ya kusafiria zikionyesha tarehe mbalimbali alizosafiri na viza alizopewa, mahojiano na vyombo mbalimbali vya habari na barua kutoka balozi mbalimbali zikionyesha kutokuwepo kwake nchini Rwanda wakati huo.
 
Hata hivyo wakati wa kuwasilisha hoja za mwisho, mwendesha mashitaka alidai kwamba ushahidi wa kutokuwapo nchini Rwanda uliotolewa na mshitakiwa umepingana na ushahidi uliotolewa na mashahidi wake mwenyewe  na wa mwendesha mashitaka.
 
Mwendesha Mashitaka Wallace Kapaya alifafanua zaidi kuwa mashahidi wa utetezi waliotoa ushahidi kuunga mkono hoja ya mshitakiwa, walikuwa marafiki zake wa karibu au jamaa zake hivyo, wana lengo la wazi kabisa la kutaka kumnusuru mshitakiwa. Alidai pia kwamba tarehe zilizoonyeshwe kwenye hati ya kusafiria zimegushiwa.
 
‘’Kutokana na kupinga huko kwa wazi na urafiki wa mashahidi hao na mshitakiwa, nawaomba muukatae ushahidi huu,’’ Kapaya alisisitiza.
 
Pande zote mbili za mwendesha mashitaka na utetezi zilihitimisha kuwasilisha hoja za mwisho na kesi kuahirishwa kwa muda usiojulikana.

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia