Ticker

6/recent/ticker-posts

JAMBAZI MMOJA AUAWA KWA RISASI AKIPORA ABIRIA


  Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha Naibu kamishna (DCP) Charles Mkumbo akitoa ufafanuzi kwa waandishi wa habari juu ya jambazi hilo lililowawa
 Na Woinde Shizza,Arusha
Mtu mmoja anayesadikiwa kuwa ni jambazi alijeruhiwa kwa kupigwa risasi na askari Polisi kisha kufariki dunia wakati akipelekwa katika hospitali ya Monduli kwa ajili ya matibabu.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo alipoongea na waandishi wa habari leo mchana ofisini kwake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha,Naibu  Kamishna (DCP) Charles Mkumbo alisema tukio hilo lilitokea muda saa 07:00 Usiku maeneo ya Makuyuni barabara ya Arusha-Makuyuni wilayani Monduli.

Kamanda Mkumbo alisema jambazi huyo akiwa na wenzake wapatao 29 walikuwa na bunduki ambayo bado haijafahamika pamoja na silaha za jadi mapanga na marungu ambapo waliweka mawe barabarani na kulisimamisha gari aina ya Fusso lenye namba za usajili T. 871 BUZ ambalo lilikuwa lina mzigo likitokea Moshi kuelekea mkoani Singida.

‘’Mara baada ya kulisimamisha gari hilo wakaanza kumpora abiria mmojawapo aliyejulikana kwa jina la Victor Pius (46) Mfanyabiashara, mkazi wa Majengo Moshi ambapo walichukua simu mbili aina ya Nokia na Samsung pamoja na fedha taslimu Tsh 50,000/=’’.
“Wakati wanaendelea na tukio hilo askari Polisi waliokuwa High Way Patrol walipata taarifa za tukio hilo ambapo walikwenda kwa haraka na mara baada ya majambazi hao kuwaona walianza kufyatua risasi hovyo na Polisi kuanza kujibu mapigo na kufanikiwa kumjeruhi mmojawao na kuwakamata wengine kumi na mbili papo hapo wakiwa na mapanga sita na marungu manne huku wengine akiwemo na yule mwenye bunduki wakikimbia”. Alifafanua Kamanda Mkumbo.
Kamanda Mkumbo alitoa wito kwa wananchi wa mkoa huu kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa kutoa taarifa za uhalifu ili zifanyiwe kazi kwa haraka, huku akitoa onyo kwa majambazi wanaopenda kujipatia kipato bila kuvuja jasho kwani Jeshi hilo limejiandaa vizuri.

Post a Comment

0 Comments