Ticker

6/recent/ticker-posts

ASKARI WATATU WA MKOANI KILIMANJARO WAFUKUZWA KAZI

WIKI moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kuagiza Jeshi polisi kuwafukuza kazi askari wote wasio waadilifu, jeshi hilo mkoani Kilimanjaro limewafukuza kazi polisi wake watatu kwa tuhuma za kufanya shughuli za udalali na kuuza mali ya mdaiwa.

Polisi waliofukuzwa kazi ni mwenye namba D.3289 Sajenti Joseph aliyekuwa dereva wa mkuu wa kituo (OCS), F.3677 PC Esebius wa Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (CID) na polisi wa kawaida mwenye namba F.6620, PC Johnson.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Absalom Mwakyoma alithibitisha kufukuzwa kazi kwa askari hao akisema hatua hiyo imetokana na kugeuka madalali na kuuza mali ya mfanyabiashara mmoja wa Rombo, Genes Shayo (34).

Ilidaiwa kuwa polisi hao waliuza mali ya mfanyabiashara huyo bila ya ridhaa yake wala kuwepo wakati wa mauziano hayo kitendo kilichodaiwa kuwa kilisababisha mfanyabiashara huyo kunywa sumu na kupoteza maisha usiku wa Februari 24, mwaka huu.
 
“Wao (polisi) walisimamia kuuza mali na fedha zilizopatikana wakamlipa mtu aliyekuwa akidaiana na marehemu na kitendo hiki, kinakiuka maadili na mwenendo mwema wa jeshi la Polisi,” alisema kamanda Mwakyoma.

Kamanda Mwakyoma, alisema polisi hao walifukuzwa kazi hiyo jana baada ya mahakama ya kijeshi kuwatia hatiani na jana walikuwa wakikabidhi mali na vifaa vya jeshi hilo.

Kufukuzwa kazi kwa polisi hao watatu wa Kituo cha Tarakea kunafanya idadi ya polisi waliofukuzwa katika kipindi cha miezi minane iliyopita kufikia 18.

Wakati akifungua mkutano wa mwaka wa jeshi hilo mjini Moshi wiki iliyopita, Rais Kikwete alisema askari asiye na nidhamu amepoteza sifa ya kuendelea kuwa mwanajeshi na ni hatari kwa usalama wa raia.

“Vitendo vya utovu wa nidhamu vinavyofanywa na baadhi ya maofisa na askari kamwe visivumiliwe… hivi majuzi nimesikia kuwa hapa Moshi askari ametoroka lindo na kwenda disko, tena akiwa na silaha, sasa huyu mtasema ni askari wenu?,” alihoji na kuongeza:

“Vitendo vya namna hii vinaleta fedheha kwa Jeshi la Polisi na kuwaacha watu wakishangaa na kuwa na maswali mengi juu ya Jeshi lao…. inawezekanaje ifikie hapo kwa askari aliyefunzwa vizuri?”

Sakata la mfanyabiashara
Baada ya kifo cha mfanyabiashara huyo, ndugu wa marehemu walikuja juu na kukataa kuzika mwili wake kwa wiki mbili hadi Machi 6, mwaka huu wakidai polisi hao wanahusika na kifo hicho.

Hata baada ya polisi hao kutimuliwa kazi, dada wa marehemu aliyejitambulisha kuwa ni Mary Shayo alifika katika Ofisi za gazeti hili mjini hapa na kusisitizia msimamo wa familia ya marehemu kutaka polisi hao washtakiwe.

“Kwanza, walimkamata kwenye saa 4:00 asubuhi na kumchukua na gari ya polisi na kumficha mahali wanapojua wao hadi saa 11:00 jioni na alipofika tu nyumbani alianguka na kufariki dunia,” alidai ndugu huyo wa marehemu.

Mary alisema kama maelezo ya polisi ni sahihi kuwa marehemu alikunywa sumu baada ya kuuzwa kwa mzigo wake wa maharagwe, basi wanatakiwa kujibu kwa kuwa alikuwa mikononi mwao muda wote.

Akizungumzia sakata hilo, Mary alidai kuwa kaka yake alikuwa akifanya biashara na mwenzake ambaye ni kiongozi wa kijiji na baadaye biashara yao iliyumba na kujikuta akidaiwa fedha na mshirika wake huyo.

Alisema mgogoro huo ulipelekwa kwa Mkuu wa Polisi (OCS) Kituo cha Tarakea na marehemu alikubali kudaiwa fedha hizo na kuahidi kulipa na hadi alipofariki dunia alikuwa ameshalipa Sh2.4milioni.

“Mara ya mwisho alilipa Sh400,000 na akamuomba OCS kwamba pesa nyingine angelipa Machi 25, mwaka huu baada ya kuuza mzigo wake wa magunia 50 ya maharagwe na OCS alikubali na kumpa siku tano,” alisema.

Hata hivyo, ndugu huyo wa marehemu alidai kuwa katika mazingira yasiyoeleweka, siku moja kabla ya tarehe aliyoahidi kulipa, polisi hao walimkamata marehemu pamoja na mzigo wake huo wa maharagwe.

Alidai kwamba baada ya polisi hao kumkamata wakishirikiana na mshirika wake huyo wa kibiashara, walimchukua marehemu na kumshikilia kwa saa nane na kuuza mazao yake hayo kwa Sh4,592,200 na fedha hizo kukabidhiwa mshirika wake.

“Tunajiuliza tangu lini polisi wakawa madalali wa mali ya mtu tena bila yeye kuwepo? Kama wanasema kitendo hiki kilimsukuma marehemu kunywa sumu, tunajiuliza alikunywa hiyo sumu mbele ya polisi?”

Dada huyo alisema baada ya polisi hao kumwachia kaka yake na kurudi nyumbani muda huo huo, alimweleza mkewe kuwa polisi wameuza mzigo wake bila yeye kuwapo na kabla ya kumaliza alianguka na kufariki dunia papo hapo.
 
Kufukuzwa kazi kwa polisi hao kumekuja wiki moja tu baada ya polisi mwingine kutimuliwa kazi kwa kuingia ukumbi wa disko akiwa na bunduki aina ya SMG.

Hili ni tukio la tatu kwa polisi kuwakamata na kuwachukulia hatua askari wake katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita. Tukio lingine ni lile lilitokea mkoani Ruvuma hivi karibuni ambako polisi wanne walikamatwa na kuswekwa rumande kwa tuhuma za kusababisha mauaji ya raia waliokuwa wakiandamana kupinga mauaji ya kishirikina.

Post a Comment

0 Comments