RASIMU ya Katiba Mpya; CHADEMA yaitisha Kamati Kuu ya dharura
Katika
hatua nyingine, CHADEMA imemtaka Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kutimiza
ahadi yake ya kuleta muswada wa marekebisho ya sheria iliyounda Tume ya
Mabadiliko ya Katiba mpya ili kuepusha mkanganyiko kwenye mjadala wa
rasimu iliyotolewa.
Msimamo wa kambi hiyo, ulitolewa jana mjini
hapa na Mbunge wa Ubungo, John Mnyika akisema kuwa Pinda ameshindwa
kusimamia maneno yake, hivyo kuruhusu Bunge kupoteza muda wa siku tano
tangu Juni 7 hadi 12 pasipo kuleta muswada huo.
“Mtakumbuka
Aprili 4 mwaka huu, Kiongozi wa kambi, Freeman Mbowe katika hotuba yake
kwa ofisi ya Waziri Mkuu alitangaza mambo mawili akitaka yatekelezwe,
vinginevyo CHADEMA ingejitoa kwenye mchakato wa katiba mpya,” alisema.
Mnyika
aliyataja mambo hayo kuwa ni kufutwa kwa mabaraza ya katiba kutokana na
uchaguzi wake kugubikwa na rushwa na hila, pili ni kuletwa kwa muswada
wa marekebisho ya sheria iliyounda Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Alifafanua
kuwa hata Msemaji Mkuu kwa Wizara ya Katiba na Sheria, Tundu Lissu
kwenye hotuba yake Aprili 30 mwaka huu, alisema wanaipa muda serikali
ilete muswada huo kabla ya rasimu kutolewa.
“Waziri Mkuu aliahidi
kutimiza sharti la pili la kuleta muswada, lakini hadi rasimu inatolewa
ameshindwa kusimama katika maneno yake. Rasimu imetoka, lakini imeibua
mjadala na ubovu wa mchakato ukiachwa utaathiri upatikanaji wa katiba
mpya,” alisema.
Aliongeza kuwa rasimu hiyo imezua mjadala kuhusu
muundo wa muungano kwa wananchi kuhoji ni kwanini rasimu inaleta muundo
huo pekee pasipo kueleza mustakabali wa katiba ya Tanganyika.
Mnyika
alieleza kuwa ubovu huo waliubaini mapema ndiyo maana viongozi wa chama
hicho walipokutana na Rais Kikwete Ikulu mwaka jana, walimweleza kuwa
sheria iliyounda tume ya katiba ibadilishwe ili hatima ya Tanganyika
iingizwe kwenye mchakato ili maoni yaguse vyote kwa pamoja.
Mnyika
alisema kuwa CCM wanajipanga katika mabaraza kujadili rasimu kwa vile
wanajua kuwa kwa mujibu wa sheria hiyo mbovu, Tume ya Mabadiliko ya
Katiba inatambua kwamba maoni yote ya mabaraza yana uzito sawa, hivyo
tume inaweza kuchakachua.
Alisema CHADEMA kwa sasa hawataki kutoa
maoni ya jumla kuhusu rasimu hiyo bali waipitie kwanza neno kwa neno
pamoja na wanachama wao nchi nzima wakilinganisha na waraka namba moja
wa mapendekezo yao kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba mpya.
“Baada
ya hapo, Kamati Kuu itakutana mwanzoni mwa Julai na kutoa uamuzi. Hata
Bunge likimaliza muda wake bila serikali kuleta muswada huo, sisi kama
kambi tutalirudisha suala hilo kwa Kamati Kuu ili kulitolea uamuzi,”
alisema.
Akigusia kwa uchache maeneo yenye kasoro kwenye sheria
hiyo, Mnyika alisema mamlaka na madaraka ya wananchi kwenye kura ya
maoni yataporwa ikiwa Tume ya Uchaguzi inayolalamikiwa itaendelea
kusimamia mchakato huo.
Pia alitaja mamlaka ya uwakilishi wa
wananchi kwenye Bunge la Katiba ambalo kwa mujibu wa sheria hiyo ukiacha
wabunge wa sasa, rais ndiye atateua wajumbe wengine baada ya kupokea
mapendekezo ya makundi mbalimbali akisema yanapokwa.
Mbowe aitisha Kamati Kuu
Katika
hatua nyingine, CHADEMA imeitisha kikao cha dharura cha Kamati Kuu
(CC), ili kujadili na kutoa msimamo wa chama hicho juu ya rasimu ya
katiba mpya, iliyotolewa hivi karibuni, huku kikiwataka wananchi wote
kuendelea kuichambua kwa makini na kutoa maoni yao kwa ajili ya
kuiboresha.
Chama hicho kimesema kuwa kikao cha Kamati Kuu
kitafanyika Jumamosi ya wiki ya kwanza, Julai mwaka huu, ambapo kwa muda
wote uliobaki kimesema kitaendelea kuichambua rasimu hiyo 'neno kwa
neno' kikisema kuwa ni muhimu kufanya hivyo kwani 'shetani hujificha
kwenye maelezo'.
Mbali ya kuwataka wananchi kuisoma kwa makini
rasimu hiyo, chama hicho pia kimewaagiza wanachama wote nchi nzima
kupitia kwenye mfumo wake wa uongozi kuanzia ngazi ya chini ambayo ni
misingi katika ngazi ya vitongoji, kuichambua rasimu kwa kuzingatia
waraka namba moja wa chama hicho juu ya maudhui ya katiba mpya ya
Tanzania, kisha wawasilishe maoni yao ili yazingatiwe kwenye maamuzi ya
kikao hicho cha Kamati Kuu.
Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa
CHADEMA, Freeman Mbowe juzi mjini Ifakara, kwenye mkutano wa kampeni ya
uchaguzi mdogo wa udiwani Kata ya Ifakara, alipokuwa akimnadi mgombea
wa chama hicho, Peter Lijualikali.
Mbowe alisema kuwa tangu Tume
ya Mabadiliko ya Katiba mpya itoe rasimu hiyo, chama hicho hakijatoa
kauli yoyote, ili kupata muda wa kuisoma na kuichambua kwa makini 'neno
kwa neno' nyaraka nzima, kisha kufanya mashauriano ya kitaalamu ndani ya
chama, huku kikifanya maandalizi ya vikao kwa ajili ya maamuzi na
hatimaye msimamo wao kwenye hatua hiyo ya mchakato wa katiba mpya.
“Ndugu
zangu wananchi wenzangu wa Ifakara, katika mkutano huu wa kampeni za
kumnadi mgombea wetu, naomba pia nitumie fursa ya kutoa tamko la kitaifa
kuhusu suala muhimu sana na nyeti la katiba mpya. Tangu Tume imetoa
rasimu ya katiba mpya, chama chenu kimekuwa kimya, kwa maana
hakijazungumza, hii ni kwa sababu kadhaa.
“Kwanza kabisa tangu
siku ya kwanza hadi leo, tumekuwa tukiipitia rasimu hiyo neno kwa neno,
kipengele kwa kipengele, maana wanasema 'the devil lies in the details'
yaani mzimu hujificha kwenye maelezo, sasa sisi kama mnavyojua tumekuwa
chanzo na chachu kubwa ya mchakato huu hadi kufikia hapa ulipo, lazima
tuwe makini katika msimamo wetu kama ambavyo imekuwa mara zote.
“Ilikuwa
lazima pia tufanye mashauriano, wataalamu wetu waangalie mambo yote ya
kitaalamu, neno kwa neno, kisha tukae vikao na kutoa msimamo wa chama
chenu. Kama mnavyojua CHADEMA si Mbowe, si Slaa, wala si mtu mwingine
yeyote, chama ni vikao. Hivyo tumeitisha kikao cha Kamati Kuu siku ya
Jumamosi, wiki ya kwanza ya mwezi wa saba, kisha tutatoa tamko na
msimamo wa CHADEMA katika rasimu hii ya katiba,” alisema Mbowe.
Aliongeza:
“Wakati tunaendelea kuipitia rasimu hii hadi Kamati Kuu ikae,
tunawataka Watanzania wote waendelee kuisoma kwa makini na kutoa maoni
yao, lakini pia kwa msisitizo mkubwa kabisa, tunawaagiza wanachama wote
wa CHADEMA katika ngazi ya msingi, kwenye vitongoji nchi nzima kukaa
vikao, kuisoma na kuichambua rasimu kwa makini, kisha watuletee maoni
yao kabla ya kikao hicho ili tuyazingatie kwenye maamuzi na utoaji wa
msimamo wetu kama chama.
“Tunawakata wanachama wetu kuipitia
rasimu yote kwa kurejea Waraka Namba Moja wa mwaka 2013 uliopitishwa na
Baraza Kuu la chama mapema mwaka huu, hasa sehemu ya pili ambayo ilikuwa
inaelezea maoni ya CHADEMA juu ya maudhui ya katiba mpya ya Tanzania.”
Mbowe
akirejea kwa kutoa mifano namna chama hicho kilivyosukuma agenda ya
katiba mpya kwa ajili ya mabadilio ya kimfumo na kiutawala kwa muda
mrefu na kuweka msisitizo kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2010, alisema
kuwa watu wengi, hasa walioko madarakani leo, waliibeza CHADEMA, lakini
leo wanakubali kuwa kiliona mbali.
Akitumia kaulimbiu maarufu ya
chama hicho 'nguvu ya umma', Mbowe aliwataka Watanzania kuendelea
kukiunga mkono katika kusimamia na kuhakikisha nchi inapata katiba mpya,
huku akisema hawako tayari kuona wakuu wa wilaya na mikoa wakiendelea
kuwemo kwenye katiba mpya.
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia