WACHIMBAJI WAOMBA KUPATIWA ZANA ZA BEI NAFUU

Wachimbaji wadogo wa madini ya Tanzanite wa Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara,wameiomba Serikali kuipatia kibali kampuni ya kizalendo ya Tan Youth Mining Ltd,ili wauziwe zana za milipuko kwa bei nafuu.

Wachimbaji hao wakizungumza juzi mbele ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini na Kaimu Mwenyekiti wake Anne Kilango Malecela walisema kampuni hiyo ikipatiwa kibali na kufutiwa kodi watachimba madini kwa urahisi. 

Mmoja kati ya wachimbaji wa madini,Abubakary Madiwa alisema kampuni hiyo chini ya Mkurugenzi wake,Mohamed Karia ingepatiwa kibali cha kuwasambazia wachimbaji wadogo zana za milipuko wangekuwa na unafuu mkubwa.

“Kampuni ya kutoka nje ya nchi ya South Africa,inatuuzia zana za milipuko kwa bei ghali hivyo tunaomba kampuni ya kizalendo ya Tan Youth Mining Ltd kupitia Mkurugenzi wake Karia ipewe kibali atuuzie kwa bei nafuu,” alisema Madiwa.

Hata hivyo,Kamishna Msaidizi wa madini kanda ya kaskazini,Benjamin Mchwampaka aliieleza Kamati hiyo kuwa alishaidhinisha kampuni ya Tan Youth Mining,ipatiwe kibali hicho ila kinachokwamisha ni makao makuu wizarani.

“Kampuni hiyo ingeweza kuwasaidia wachimbaji wadogo kwa suala la milipuko na nilishasaini yote yanayonihusu,ila wizarani bado hawajasaini na alishahojiwa mpaka na kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa,” alisema Mchwampaka.

Akizungumzia kuhusu hilo,Kaimu Mwenyekiti wa kamati hiyo,Anne Kilango Malecela aliwataka wachimbaji hao kuandika barua kwenye kamati hiyo wakutane na wizara mwezi ujao ili kampuni hiyo ipatiwe kibali hicho.

“Kama mnaona kampuni hiyo ya kizalendo, itawanufaisha wachimbaji wadogo kwa kuwezesha upatikanaji na unafuu wa bei ya zana za milipuko andikeni barua sisi tutawasaidia kwa kuwakutanisha na wizara,” alisema Malecela.

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post