Ticker

6/recent/ticker-posts

VIONGOZI WA DINI WATAKIWA KUTOWARUHUSU WANASIASA KUTUMIA MADHABAHU YAO



Viongozi wa dini hapa nchini wametakiwa kutoruhusu wanasiasa kuyatumia madhabahu yao na nyumba za ibada kuzungumzia mambo ya kisiasa katika wakati huu wa uchaguzi ili kuilinda amani hapa nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Jukwaa la wakristo hapa nchini na  Askofu wa kanisa la Aglikana la mt.Kilimanjaro Stanley Hotay kwenye kongamano la mbegu ya amani Tanzania  lililofanyika jijini hapa na kuwashirikisha viongozi wa madhehebu ya kikristo kanda ya kaskazini.

Alisema kuwa mimbari zetu zisitumiwe kinyume cha sheria kwa kuwaelekeza waumini wao kuhusu mgombea ama chama cha siasa cha kukichagua wao wapewe uhuru wa kufanya maamuzi yao ni yupi wa kumpa kura zao kwa kuwa wanasiasa hao wote ni waumini wao.
Aliwataka viongozi hao wa dini kukataa rushwa za pesa,na bakshishi zingine kwa ahadi ya kulindwa na kupewa nyadhifa za kuteuliwa iwapo wanasiasa hao watapata nafasi hilo ni suala la kuliepuka kabisa.

‘’Mikusanyiko sio kipindupindu tukatae kusimama kwenye majukwaa ya kisiasa kuwanadi wagombea na pia kwenye nyumba zetu za ibada kutompigia debe mwanasiasa yeyote hiyo itatuepusha na kuvuruga haki ya waumini wetu ya kujichagulia wanaomuona anawafaaa’’alisema Hotay.

Aidha alilitaka jeshi la polisi hapa nchini kupitia kwa mkuu wa jeshi hilo Ernest Mangu kuangalia kutenganisha Maandamano,Mikutano ya hadhara na mikusanyiko mbali mbali ya kidini na kisiasa kwamba vibali vya mikusanyiko ya kisiasa wapewe wakuu wa polisi na vibali vya mikusanyiko ya kidini wapewe wakuu wa wilaya.

Alisema kuwa hilo litaepusha jeshi la polisi au waziri kutoa adhabu ya jumla na kusababisha viongozi wa dini pamoja na waumini wao kujenga chuki kubwa kwa serikali yao na kusababisha viongozi wa kidini kufikia kuzungumzia katika vikao vya mara kwa mara kwamba serikali inaagenda ya siri na viongozi wa dini.

Alikemea siasa za matusi na kuchafuana katika majukwaa na badala yake aliwataka kutumia lugha za staha na kuheshimiana,huku akiwataka kutoa uhuru wao wa siku ya jumapili kuabudu badala ya kuifanya ndio siku ya uchaguzi.

Post a Comment

0 Comments