Ticker

6/recent/ticker-posts

WAMTAKA AGOMBEE UBUNGE

Wananchi wa Wilaya ya Rorya, Mkoani Mara, wanaoishi Mji mdogo wa Mirerani Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wamemuomba Mwenyekiti wa Chadema jimbo la Rorya, Charles Odero agombee ubunge wa jimbo la Rorya.

Wakizungumza juzi mji mdogo wa Mirerani, wananchi hao walisema kupitia umoja wao ikiwemo Mara Group wapo tayari kumuunga mkono Odero kwani ni kijana mwenye maono na uwezo wa kufuatilia na kutatua matatizo ya jamii.

Thobias Magati alisema atamuunga mkono Odero kwa kuwahamasisha ndugu zake waliopo Rorya kwani jimbo hilo liliongozwa na watu wenye ulimu ya kawaida, mwanasheria, profesa na sasa ni wakati wa mwinjilisti aongoze Rorya.

“Kupitia Odero wale watu wanaoturudisha nyuma kwa kudai kuwa wanafikiria kwa kutumia tumbo na siyo akili tutawakomesha, tuendelee kupambana ili sasa hivi wajitambue na siyo kujali fedha wanazopewa,” alisema Okuku Obata.

Naye, Odero alisema yupo tayari kugombea ubunge jimbo la Rorya na anaamini uongozi shirikishi kwa kuwa mbele yao, katikati na nyuma yao kwa kuwalinda kuwasikiliza na kuwaonyesha njia ya kuwafikisha mbali kwenye maendeleo.

“Jimbo la Rorya lina fursa nyingi ikiwemo ziwa Victoria, ardhi yenye rutuba na kuwa mpakani na Kenya, hivyo hatuhitaji mbunge aliyetuna mifuko ila tunahitaji mbunge mwenye maono na upeo wa kuona mbali,” alisema Odero.

Alisema kutokana na Rorya kukosa mbunge makini, wananchi wamekosa fursa nyingi za maendeleo ikiwemo shule za serikali za sekondari zenye kidato cha tano na sita, barabara nzuri, elimu bora, maji safi na vituo vya afya.

“Tutawakomesha wale wanaodhani fedha ndiyo inawapa uongozi kwani tuumefanikiwa kufanya vizuri kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka jana hivyo tutashinda ubunge na kupata madiwani wengi zaidi yao,” alisema Odero.

Post a Comment

0 Comments