Ticker

6/recent/ticker-posts

HII NDO TWASIRA YA AJALI YA WAANDISHI WA HABARI ILIYOTOKEA ARUSHA JANA

WAANDISHI wa habari sita wamenusurika kufa baada ya gari walilikuwa wakilitumia kwenye msafara wa wabunge wa Umoja wa Kamati za Mabunge za Hesabu za Serikali kutoka nchi Wanachama wa SADC (SADCOPAC), kuanguka wakiwa njiani kuelekea Hifadhi ya Ngorongoro.
Ajali hiyo ilitokea jana saa 3:30 asubuhi nje kidogo ya mji wa Karatu ambapo waandishi waliokuwemo na vyombo vyao kwenye mabano ni Veronica Mheta (Habari Leo), Asraji Mvungi (ITV), Edwin Mjwahuzi (Mwanachi), Peter Nyanje (Citizen), Deogratius Kasamia (Cluods Tv) na Afisa Habari wa Bunge, Owen Mwandumbya.
Gari hilo lenye namba za usajili T731 ARL lilikuwa likiendeshwa na dereva wa kampuni ya uwakala wa utalii Shidolya Tours & safari aliyejulikana kwa jina moja la Riziki ambaye alipoteza fahamu.
Kwa mujibu wa waandishi hao, mara baada ya tukio hilo walipatiwa usafiri wa kuwapeleka mpaka Hospitali ya Wilaya ya Karatu kwa matibabu ambapo baada ya uchunguzi wengine walionekana wako sawa, hivyo kuendelea na safari Majeruhi wengine, Kasamia, Oweni, dereva, Riziki na ofisa usalama ambaye jina lake halikupatikana walipelekwa jijini Arusha kwa matibabu zaidi baada ya kuonekana wana majeraha.
Kamanda wa polisi mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alisema kuwa alisikia tukio hilo ingawa bado anasubiri taarifa kamili toka kwa mkuu wa polisi wa wilaya hiyo ili aweze kutoa taarifa kwa vyombo vya habari.
Wakielezea tukio hilo, waandishi hao walisema kuwa gari lao likiwa katika msafara wa magari zaidi ya 50 yaliyobeba wabunge, askari na wanausalama lilijaribu kulipita gari lililokuwa mbele ndipo ghafla gari jingine lililokuwa kwenye msafara nalo lilitoka kwa mwendo kasi likiyapita magari mengine.
Mheta alisema kuwa hali hiyo ilimfanya dereva wa gari lao kupoteza muelekeo ambapo alijaribu kuwakwepa waenda kwa miguu waliokuwa pembeni ya barabara lakini alishindwa kulimudu na hivyo likapinduka.
Chanzo: Tanzania Daima, Picha zote na Owen David

Post a Comment

0 Comments