Rais Jakaya Kikwete, amesema serikali yake inalifanyia mageuzi muhimu na
marekebisho makubwa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) kwa nia ya
kuharakisha jitihada za serikali kusambaza umeme kwa wananchi wengi
zaidi.
Rais Kikwete aliyasema hayo jana alipokutana na kuzungumza na ujumbe wa
Shirika la Misaada ya Maendeleo la Marekani la Millennium Challenge
Corporation (MCC) ukiongozwa na Mtendaji Mkuu wake, Daniel Yohannes.
Yohannes alimwelezea Rais Kikwete kuhusu maendeleo ya ombi la Tanzania
kuingizwa katika awamu ya pili ya misaada ya Serikali ya Marekani
kupitia MCC chini ya Akaunti ya Milenia Tanzania (MCA(T)).
Nchi nyingine za Afrika ambazo maombi yao yanafikiriwa katika awamu hiyo ya pili ni Morocco, Msumbiji na Lesotho.
Tanzania ndiyo nchi iliyopokea sehemu kubwa zaidi ya msaada wa MCC
duniani katika awamu ya kwanza ambapo ilipewa dola milioni 698 za
Marekani.
Fedha hizo zimeingizwa katika miradi mikubwa ya ujenzi wa barabara,
usambazaji wa umeme vijijini, miradi ya maji na ujenzi wa Uwanja wa
Ndege wa Mafia.
Serikali ya Tanzania imeamua kuwa fedha za awamu ya pili ya MCC,
zitaingizwa kupanua zaidi huduma za umeme na ujenzi wa barabara za
vijijini kwa nia ya kuongeza idadi ya Watanzania wanaopata huduma za
umeme na kwa nia ya kuboresha barabara za vijijini katika maeneo
yanayozalisha mazao kwa wingi zaidi.
Serikali imeliweka suala la usambazaji umeme kwa Watanzania mijini na vijijini miongoni mwa maeneo yake ya kipaumbele.
Wakati anaingia madarakani mwaka 2005, ni asilimia 10 tu ya Watanzania waliokuwa wanapata umeme.
Yohannes alitaka kujua ni hatua zipi serikali inazichukua kurekebisha
changamoto zinazoikabili Tanesco na hatua zinazochukuliwa kuzidi
kukabiliana na matatizo ya rushwa.
Rais Kikwete alimweleza Yohannes: “Kama unavyojua, Tanesco imepitia
safari ngumu na kukabiliwa na changamoto nyingi, lakini sasa tumeamua
katika serikali kulifanyia mageuzi muhimu na marekebisho makubwa kwa
maana ya muundo wake na pia kuangalia viwango vya malipo ambayo shirika
hilo linawatoza wateja wake. Mageuzi haya katika Tanesco ni muhimu sana
na yameanza kufanyika na kwa hakika serikali imedhamiria kukayamilisha
mageuzi hayo katika muda mfupi iwezekanavyo.”
0 Comments
unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia