Ticker

6/recent/ticker-posts

TIMU YA SIMBA YAZURU TANZANITE ONE

Baada ya timu ya soka ya Simba SC ya jijini Dar es salaam jana kucheza ligi kuu ya Vodacom na Oljoro JKT jijini Arusha, leo wanatarajia kutembelea machimbo ya madini ya Tanzanite ya mji mdogo wa Mirerani wilayani Simanjiro Manyara.

Akizungumza na gazeti hili, Ofisa mahusiano wa kampuni ya TanzaniteOne, Khalifan Hayeshi alisema timu ya Simba baada ya kufika kwenye machimbo hayo itatembelea na kujionea namna shughuli za uchimbaji zinavyoendelea.

“Ni ziara ya kutalii kwenye eneo letu na lengo ni kufahamu namna madini ya Tanzanite yanavyochimbwa na kupatikana hivyo tunatarajia leo alhamisi watakuwa hapa kwetu TanzaniteOne,” alisema Hayeshi.

Naye, Mkurugenzi wa timu ya soka ya Tanzanite FC, Jofrey Nyigu (Mnyalu) alisema baada ya timu ya Simba kutoka kutembelea migodi ya madini ya kampuni ya TanzaniteOne watafika mji mdogo wa Mirerani kuiona timu yake.

“Pia watafanya mazoezi na timu yetu jioni, kabla ya kwenda kuweka mwili vizuri kwenye sehemu mpya ya Nicks Barbershop hapa mji mdogo wa Mirerani kisha wataondoka kwenda jijini Dar es salaam,” alisema Nyigu.

Kwa upande wake, Makamu Mwenyekiti wa timu ya Simba Joseph Itangare (mzee Kinesi) alithibitisha timu yake kufanya ziara ya kutembelea mji mdogo wa Mirerani mkoani Manyara.

“Baada ya leo (jana) kucheza mechi yetu na JKT Oljoro tunatarajia kesho (leo) kutembelea machimbo ya madini ya Tanzanite na kufanya utalii wa ndani mji mdogo wa Mirerani kabla ya kurudi jijini Dar es salaam,” alisema.

Post a Comment

0 Comments