Ticker

6/recent/ticker-posts

MAOFISA WA POLISI WALIOSHUSHWA VYEO NA NCHIMBI HAWA HAPA

Picha  juu na chini ni sehemu ya wafuasi wa chadema wakitimua mbio leo muda mfupi baada ya jeshi la polisi mkoani arusha kuwatawanya wakati wafuasi wa chadema walipotaka kuanza kuaga miili ya watu waliofariki kwenye mlipuko wabomu kwenye mkutano wa chadema

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi amewavua madaraka maofisa wanne wa polisi kwa kushindwa kuwajibika ipasavyo, huku akiwafukuza kazi askari saba wa vyeo vya chini pamoja na kuwapa onyo wawili kutokana na kushiriki moja kwa moja katika matukio ya wizi, kusababisha mauaji na uzembe kazini.
Nchimbi alipoulizwa sababu za kutowafukuza kazi maofisa wa juu, badala yake amekuwa akiwavua madaraka alisema, “Hawa niliowataja sio kama wanahusika, tunawavua madaraka kwa sababu ya kushindwa kusimamia majukumu yao kikamilifu. Madaraka waliyopewa yamewashinda hivyo tumewanyang’anya.”
Maofisa waliovuliwa madaraka ni Mkuu wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) mkoani Arusha, Mrakibu wa Polisi Ramadhan Giro, Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Mvomelo, Jamal Ramadhan, Mkuu wa Kituo cha Polisi Dumila, Juma Pamba na Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kasulu, Daniel Bendarugaho.
Hii ni mara ya pili kwa Dk Nchimbi kuwachukulia hatua maofisa wa polisi, kwani Machi mwaka huu waziri huyo aliwafukuza kazi maofisa watano wa polisi na kumsimamisha kazi kwa mwezi mmoja Kamishna msaidizi mwandamizi wa jeshi hilo, Renatus Chalamila kutokana na kuhusishwa na rushwa katika kuajiri.
Pia aliwafukuza makuruta 95 waliokuwa Chuo cha Polisi (CCP), Moshi kutokana na kugundulika kutumia rushwa kupata ajira.
Maofisa watatu kati ya hao watano walifukuzwa kutokana na kugundulika kuwa walikamata dawa za kulevya aina ya cocaine lakini zilipopelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali ziligundulika ni chumvi na sukari.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Dk Nchimbi alisema amechukua hatua hiyo baada ya kupata ripoti ya kamati aliyoiunda kuchunguza matukio yaliyotokea kati ya Desemba 26 mwaka jana na Mei 18 mwaka huu.
Alisema matukio hayo ni lile la gari la FFU kutumika kubeba bangi mkoani Kilimanjaro, polisi kutumia fuvu la kichwa cha binadamu kumbambikizia mfanyabiashara kesi kwa lengo la kupata fedha mkoani Morogoro pamoja na mauaji ya mfanyabiashara wilayani Kasulu yaliyofanywa na askari wawili.
Sababu za kuvuliwa madaraka
Alisema Giro amevuliwa madaraka kutokana na kushindwa kusimamia kikamilifu askari na maofisa walio chini yake na kusababisha Mei 18 mwaka huu, kutumika kwa gari la polisi lenye namba za usajili PT 2025 kubeba bangi kilogramu 540 zenye thamani ya Sh81 milioni.
“Yeye ndiye msimamizi wa magari yote ya FFU na ndiye mkuu wa kikosi hicho katika mkoa huo, kwa utaratibu wa magari ya FFU hayaendi popote bila yeye kujua, ikitokea hakujua na mpaka gari limevuka nje ya mkoa maana yake hakutimiza wajibu wake ipasavyo, kamati ilishauri avuliwe madaraka,” alisena na kuongeza;
“Nilipoipata taarifa ya kamati juzi niliagiza polisi wamvue madaraka na hilo lilifanyika siku hiyohiyo.”

Post a Comment

0 Comments