Ticker

6/recent/ticker-posts

KESI DHIDI YA MMILIKI WA HOTELI YA SNOWCREST JIJINI ARUSHA YAHAIRISHWA TENA



KESI ya madai inayomkabili mfanyabiashara  ambaye pia ni mmiliki wa hoteli ya Snowcrest jijini Arusha,Wilfred Tarimo imehairishwa tena juzi katika mahakama ya biashara kanda ya Arusha hadi desemba 14 mwaka huu mara baada ya upande wa mdaiwa kukataa  kulipa kiasi cha fedha na riba anachodaiwa katika kesi hiyo.

Kesi hiyo  nambari 9 ya mwaka 2012  mkurugenzi wa kampuni ya Grand Alliance Limited,James Ndika amefungua madai dhidi ya mmiliki wa hoteli ya Snowcrest Hotel and Wildlife Safaris Ltd  ambaye ni Tarimo ambapo katika shauri hilo mdai analalamika kutapeliwa jumla ya kiasi cha $ 1.7 milioni sawa na sh,3  bilioni  kwa ajili ya mauziano ya hoteli hiyo.

Katika kesi hiyo mlalamikaji anadai  kwamba mmiliki huyo wa Snowcrest alimuuzia hoteli hiyo mnamo novemba mwaka  2011 na kumpatia hati mbili za eneo la hoteli hiyo lakini baadaye ilikuja kugundulika kwamba eneo la hoteli hiyo lina hati tatu .

Katika kesi hiyo mlalamikaji amedai kwamba hati moja kati ya hizo tatu ina mkopo wa kiasi cha sh,1.5 bilioni kupitia benki mojawapo hapa nchini ambapo mara baada ya kubainika ilikwamisha biashara ya mauziano ya hoteli hiyo.

Katika shauri hilo Ndika anaomba alipwe kiasi chote cha fedha alizotoa kwa ajili  ya kuinunua  hoteli hiyo sanjari na riba tangu siku ya mauziano kwa kuwa mmiliki wa hoteli hiyo alimdanganya na kumpatia hati mbili lakini kumbe  badala yake ina hati tatu.

Mbele ya jaji anayesikiliza shauri hilo, Nyangarika alisema kwamba mara baada ya hatua ya usuluhishi kukwama katika kesi hiyo kufuatia upande wa mdaiwa kukataa kulipa kiasi hicho cha fedha na riba kwa mamlaka aliyonayo  ameamua kuiharisha kesi hiyo hadi desemba 14 mwaka huu hadi pale mahakama itakapopanga tarehe ya kuanza kuisikiliza .

Mara baada ya jaji Nyangarika kutoa kauli hiyo aliwauliza mawakili wa pande zote mbili endapo wamekubalina na uamuzi wake na ndipo walipotamka kwa nyakati tofauti kwamba hawana pingamizi juu ya  kauli hiyo na kisha  kesi hiyo  kuharishwa .

Katika kesi hiyo upande wa mlalamikaji unawakilishwa na wakili Melkizedeck Lutema huku upande wa mlalamikiwa unawakilishwa na wakili,Nelson Merinyo.

Post a Comment

0 Comments