CHUO CHA UALIMU MONDULI CHAHAIDI KUBORESHA MICHEZO

CHUO cha Ualimu Monduli mkoani Arusha, kimeazimia kuboresha michezo shuleni kwa kuzalisha walimu waliofundishwa mbinu mbalimbali za kuibua na kukuza vipaji kwa wanafunzi.
Walimu hao watakuwa wakifundisha michezo kama masomo ya kawaida, badala ya mfumo wa sasa wa michezo kuwa kama vipindi vya ziada baada ya masomo.
Akizungumza kwenye uwanja wa michezo wa kumbukumbu ya Sheikh Amri Abeid hivi karibuni, mkufunzi wa michezo chuoni hapo, Lamon Mtweve, alisema katika kutekeleza hilo, uongozi umeendesha kozi maalumu kwa walimu wenye mwamko wa michezo, ili wakatumike katika shule watakazokwenda kufundisha kwa ajili ya kusimamia michezo na kukuza sekta hiyo ambayo imekuwa ikifanya vibaya katika siku za hivi karibuni.
“Hii kozi tunayofundisha si tu kwa ajili ya kwenda kuwafundisha wanafunzi masuala ya michezo mashuleni, bali pia itawasaidia walimu watakaowakuta huko kufaidika, hasa wale waliosoma nje ya chuo chetu ambao hawajasoma michezo wala hawaijui,” alisema.
Aliongeza kuwa kwa upande wa wanafunzi watajifunza michezo ya aina mbalimbali, badala ya kushiriki ile iliyozoeleka kama soka na netiboli, kwani walimu hao wanaandaliwa kuwa wataalamu wa michezo ya aina mbalimbali kama riadha, tenisi, wavu, mikono, kuogelea, n.k.

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post