NASSARI AITAKA SEREKALI INUNUE MASHINE ZA KIELETRONIKI NCHINI ZINAZOUZWA KWA BEI RAISI

 

MBUNGE wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (CHADEMA), ameihoji serikali ni kwanini isinunue mashine za kieletroniki (EFD) nchini China ambako zinauzwa kwa bei ndogo.
Nassari amehoji hatua hiyo bungeni jana alipokuwa akiuliza swali la nyongeza na kusema kuwa mashine hizo nchini China zinauzwa kati ya dola 50 hadi 100.
Akijibu swali hilo, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, alisema mashine zinazoagizwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), zina kiwango na ubora na kwamba zina uwezo wa kutunza kumbukumbu.
Katika swali la msingi, Mbunge Viti Maalumu, Rita Kabati (CCM), amehoji serikali kama haioni kuna umuhimu wa kutoa elimu ya kutosha kwa walengwa kabla ya kuanza kutumia mashine zao.
Pia alitaka kujua ni kwanini serikali isiwe na mpango wa makusudi wa kupunguza bei ya mashine hizo au kutoa ruzuku kwa kuzingatia malalamiko ya wafanyabiashara.
“Mfumo wa kutumia mashine za Kieletroniki (EFD), ni mpya katika nchi yetu na bado haujaeleweka vizuri kwa wafanyabiashara na ndiyo maana kumekuwa na migomo ya wafanyabiashara kwenye baadhi ya maeneo nchini,” alisema mbunge huyo.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, alisema mfumo wa kutumia mashine za kielektroniki za kutolea risiti (EFD), ulianza rasmi nchini Julai mwaka 2010, umekuwa ukitekelezwa kwa awamu.
“Katika kuanzisha mfumo huu TRA ilianza kutoa elimu kwa wafanyabiashara waliolengwa kutumia katika awamu ya kwanza ambao walikuwa ni wafanyabiashara waliosajiliwa kulipa kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
Akizungumzia malalamiko ya wafanyabiashara kuhusu bei ya mashine hizo, alisema serikali imeyafanyia kazi malalamiko hayo na kushusha bei kutoka sh 600,000 na 800,000 za awali hadi kufikia kati ya sh 600,000 na 690,000 kulingana na aina ya mashine.

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

Previous Post Next Post