Ticker

6/recent/ticker-posts

MKUU WA WILAYA AAGIZA MITI ISIKATWE

MKUU wa Wilaya ya Hanang’ Mkoani Manyara,Christina Mndeme amepiga marufuku ukataji miti hovyo kwenye wilaya yake kwa ajili ya matumizi ya uchomaji wa mkaa na uharibifu wa mazingira.

Mndema alitoa agizo hilo juzi,kwenye kijiji cha Getanuwas wakati akizindua matumizi ya mkaa mbadala uliotengenezwa na kikundi cha wanawake 27 wa kikundi cha Umoja cha kata ya Getanuwas wilayani humo.

Mndeme alisema atawachukuliwa hatua kali watakao kata miti hovyo kwani jamii ya wa mkoa huo inatakiwa kutumia mkaa huo mbadala kuliko kukata miti hovyo kwani wanaharibu mazingira ya wilaya hiyo. 

“Huu mkaa mbadala ni mzuri na unatengenezwa hapa kwetu Hanang’ hivyo tunatakiwa tuwaunge mkono wote walioubuni kwa kuutumia kwani hata mimi nautumia mkaa huo ambao kipande kimoja kinauzwa sh200,” alisema Mndeme.

Pia mkuu huyo wa wilaya alijitolea sh300,000 ili kukiwezesha kikundi hicho mashine ya kutengeneza mkaa huo mbadala kwani mashine wanayotumia hivi sasa ni mali ya Dayosisi ya Mbulu,inayotumiwa kwa mafunzo sehemu nyingine.

Naye,Mratibu wa mradi wa kuondoa umaskini na kukuza uchumi mkoani Manyara,Goma Gwaltu alisema mradi huo umewezeshwa na shirika la misaada ya makanisa ya Kinorway (NCA) kupitia kanisa la KKKT Dayosisi ya Mbulu.

Gwaltu alisema kuwa mradi huo wa kutengeneza mkaa mbadala (Briquettes) utawanufaisha wanawake hao kiuchumi na pia utamaliza tatizo la uharibifu wa mazingira kwenye wilaya hiyo.

Alisema matarajio yao ni kuutangaza mradi huo mkoa mzima na teknolojia hiyo ikienea sehemu tofauti itanufaisha kikundi hicho kwa kutumia nishati mbadala inayotokana na nyasi,karatasi na majani yaliyoanguka toka mitini.

Kwa upande wake,Askofu wa Dayosisi ya Mbulu iliyodhamini mafunzo ya mradi huo,Zebedayo Daudi alisema jamii ya eneo hilo inapaswa kubadilika ili kutunza mazingira kwa kutumia mkaa huo mbadala na kuachana na ukataji miti.

“Kijiji kiliitwa Getanuwas na jamii ya wabarbeig kwa kiswahili ni mti mfupi hivyo badilikeni kwa kutunza mazingira na soko la mkaa huu mbadala litakuwepo tu kwani hata Dar es salaam wanahitaji huduma hii,” alisema Askofu Daudi.

Post a Comment

0 Comments