Ticker

6/recent/ticker-posts

MADIWANI HAI WACHACHAMAA NA MAKOSA YA UANDISHI

BARAZA la Madiwani wilayani Hai, limeelezea kutoridhishwa na uandaaji wa kumbukumbu za vikao mbalimbali unaofanywa na wataalamu, hali inayochangia kutumia muda mwingi kufanya marekebisho.
Wakizungumza kwenye kikao cha baraza, madiwani walitaka uongozi wa halmashauri hiyo kueleza sababu ya kuendelea kuongezeka kwa makosa ya kiuandishi kwenye mihtasari mbalimbali ya vikao, hivyo kusababisha kutumia muda mwingi wa vikao kufanya masahihisho.
Madiwani walitaka kujua kama mihtasari hiyo baada ya kuandaliwa na watendaji kama  inapitiwa pia na timu ya wataalamu ya wilaya (CMT), ili kupunguza makosa hayo yanayoonekana.
Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Melkizedeki Humbe, alisema suala hilo hawezi kulizungumzia kwenye kikao hicho, ila tayari anazo hatua binafsi atakazochukua kuhusiana na wahusika.
“Kuhusu makosa na usahihishaji naomba kwa ridhaa yako kwa leo nisilitolee uamuzi hapa, ila ninajua hatua binafsi ambayo mimi nitachukua ila sitazungumzia kwenye baraza kwa sababu ya wahusika,” alisema.
Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Clement Kwayu, alisema mkurugenzi amekwishayaona madhaifu hayo kutokana na kuwepo kwa maswali mengi juu ya kuongezeka kwa makosa katika uandaaji wa taarifa muhimu za vikao vya baraza.

Post a Comment

0 Comments