Ticker

6/recent/ticker-posts

KIKWETE AFUNGUA RASMI OFISI MPYA YA TRA MJINI KARATU


Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete, Mbumge wa Karatu mchungaji Israeli Nase(Watatu kushoto),Waziri wa Maji Profesa Jumanne Maghembe(Wapili kushoto),Mkuu wa Mkoa wa Arusha Magesa Mulongo(kushoto) na Mkurugenzi wa Utumishi na utawala wa TRA aliyemwakilisha Kamishna mkuua wa TRA Bwana Abubakari Kunenge(wapili kulia) na kulia ni mwakilishi wa ofisi ya TRA Mkoa Bi.Caroline Ntinku. Rais Dkt.Jakaya Mrisho Kikwete akifunu kitambaa katika jiwe la msingi kuashiria kufungua rasmi ofisi ya Mamlaka ya mapato Wilaya ya Karatu leo mjini Karatu. 


RAIS Jakaya Kikwete amesisitiza msimamo wa Serikali, kwamba mashine za elektroniki za ukusanyaji kodi (EFDs), lazima ziendelee kutumika nchini. Alisema hayo jana wakati alipozungumza kwenye uzinduzi wa Ofisi za Mamlaka ya Bandari (TRA) mjini Karatu katika Mkoa wa Arusha, na kuongeza kuwa changamoto za mashine hizo zinajadilika.
“Najua kuna maneno mengi kuhusu suala hili. Kwa hiyo maelekezo yangu ni kwamba kaeni chini, mjadili matatizo yaliyopo na kupata ufumbuzi. Kama ni suala la bei pia linazungumzika lakini tunahitaji mfumo huu wa malipo ya kodi,” alisema.

Aliagiza viongozi wa TRA kukaa chini na wadau na watumiaji wa mashine hizo kuzungumza na kutafuta majawabu yanayolalamikiwa na wadau.
Alisema kuacha kutumia mashine hizo ni kurudi nyuma kwa kuwa zimeshaanza kutumika duniani kote na hata nchi jirani baadhi zimeshaanza kutumia na nyingine ziko katika maandalizi ya kutumia.
“Kwenye hili tusirudi nyuma kwa sababu tukifanya hivyo, tutakuwa tunarudi nyuma sana kwa sababu dunia nzima inaelekea huko na hata majirani zetu wote ama wameanzisha mfumo huo ama wanajiandaa kuuanzisha.”
“Hatuwezi kurejea kwenye mfumo ule wa kutumia vijirisiti. Mfumo wa sasa unaifanya kazi ya kukusanya kodi kuwa rahisi kwa Serikali yenyewe na kwa walipa kodi. Najua watu hawapendi kulipa kodi lakini hakuna njia ya jinsi ya kuendelea isipokuwa kwa kulipa kodi,” alisisitiza Rais Kikwete.
Kwa muda mrefu TRA imekuwa ikisisitiza kuwa utaratibu wa kutumia mashine za EFDs ulianzishwa kwa lengo la kumrahisishia mfanyabiashara utunzaji wa kumbukumbu za biashara za kila siku pamoja na kuondoa usumbufu wakati wa ukadiriaji wa kodi. Mfumo huo wa kutumia mashine za kodi za kielektroniki ulianza kutekelezwa kwa awamu.
Awamu ya kwanza ilianza mwaka 2010 kwa wafanyabiashara waliosajiliwa kwenye kodi ya ongezeko la thamani (VAT).
Awamu ya pili ilianza 2013 ikiwahusu wafanyabiashara ambao hawajasajiliwa kwenye VAT ambao mauzo ghafi kwa mwaka ni Sh milioni 14 na zaidi.
Kwa mujibu wa taarifa za TRA, wafanyabiashara zisizo rasmi zikiwemo za mama lishe na wale wanaotembeza bidhaa barabarani, hawahusiki kwa sababu hawana sehemu maalumu ya kufanyia biashara.
Miongoni mwa wafanyabiashara wanaotakiwa kutumia mashine hizo ni wenye maduka ya vipuri, mawakili, maduka ya jumla, wafanyabiashara wakubwa wa mbao, migahawa mikubwa, maduka ya simu na vipuri vyake, baa na vinywaji baridi, studio za picha, biashara za kutoa huduma za chakula, wauzaji wa pikipiki, maduka makubwa ya nguo na biashara zinginezo Kwa mujibu wa taarifa za TRA, kwa nchi nzima walengwa ni wafanyabiashara laki mbili tu kwa awamu ya pili kati ya wafanyabiashara zaidi ya milioni moja na nusu ambao wamesajiliwa kulipa kodi.
Rais Kikwete alikuwa katika ziara ya siku moja kukagua shughuli za maendeleo wilayani Karatu katika Mkoa wa Arusha na jana na leo ameanza  ziara kama hiyo ya siku moja katika Wilaya ya Mwanga, Mkoa wa Kilimanjaro. 

Post a Comment

0 Comments