Ticker

6/recent/ticker-posts

MECHI YA YANGA NA JKT OLJORO WAANGUKIA PUA MAPATO KIDUNCHU

WADAU wa michezo mkoani Arusha wamesikitishwa na uchakachuaji wa mapato katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Oljoro JKT na Yanga ulioingiza sh milioni 25.3.
Katika mechi hiyo Yanga iliibuka na ushindi wa mabao 2-1.
Kwa uwezo wa Uwanja wa Sheikh Amri Abeid Kaluta na idadi ya watu walioingia kwa kiingilio cha sh 5,000 na 15,000 imeonekana dhahiri uchakachuaji ulikuwa mkubwa na hali hii inazidi kuwakatisha tamaa wadau wa soka mkoani Arusha.
Uwezo wa Uwanja wa Sheikh Amri Abeid ni watu 13,000 ukijaa na mahudhurio ya juzi mashabiki waliojitokeza wanakadiriwa kufikia asilimia 75 ya uwanja, ambao ni kadirio la watu zaidi ya 9,000, ambayo ukizidisha kwa kiingilio cha sh 5,000 ni sh milioni 45 achilia mbali watu 900 waliokaa jukwaa kubwa ambalo kiingilio chake kilikuwa ni sh 15,000.
Alipoulizwa juu ya mapato hayo, Katibu wa Chama cha Soka Mkoa wa Arusha (ARFA), Adam Brown, alisema ni kweli mchezo huo uliingiza sh milioni 25 lakini hakuwa na mnyambulisho wa makato, kwani jukumu hilo liko chini ya mweka hazina wa chama na msimamizi wa kituo.
Uchunguzi wa LIBENEKE LA KASKAZINI umebaini baadhi ya mgawanyo wa mapato hayo kuwa ni pamoja na kila timu kuambulia sh 5,327,319 Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), sh 3,940,000, mfuko wa maendeleo ya ligi (FDF), sh 892,757 gharama za kuchapa tiketi sh 1,755,000, Bodi ya Ligi sh 1,755,000 na gharama za mchezo sh 1,700,000.
Hata hivyo, Brown amekiri watazamaji kuwa wachache, kulikochangiwa na ukweli kwamba, Oljoro walikuwa wanashuka daraja na Yanga walishapoteza uwezo wa kutetea ubingwa na mashabiki wengi walikwenda kushuhudia pambano la Ligi ya Uingereza kati ya Liverpool na Manchester City lililokuwa likioneshwa kwenye runinga.
“Ili kurejesha imani kwa mashabiki wa soka, lazima sekta husika kufanyia kazi mapato ya viingilio uwanjani, kwani bila hivyo inakatisha tamaa kwa wadau, mashabiki na hata wachezaji,” alisema shabiki aliyejitambulisha kwa jina moja la Jumanne

Post a Comment

0 Comments