BREAKING NEWS

Wednesday, April 2, 2014

HII NI AIBU KWA TAIFA WATANZANIA MILIONI 14 KUTOJUA KUSOMA NA KUANDIKA

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi.Dk Shukuru kawambwa

Wiki iliyopita tulichapisha habari ya kushtusha kwamba Watanzania milioni 14 hawajui kusoma wala kuandika. Ni habari ya kushtusha kwa sababu idadi hiyo ya wananchi mbumbumbu ni kubwa mno, kwa maana kwamba ni sawa na asilimia 33 ya Watanzania wote ambao ni milioni 44. Huu ni uthibitisho kwamba tumepoteza dira na mwelekeo kama taifa kwa kushindwa kutambua vipaumbele vya taifa, badala yake tukaelekeza rasilimali nyingi katika mambo yasiyokuwa na tija kwa ustawi na maendeleo ya nchi yetu.
Takwimu hizo za kushtusha zinatokana na ripoti iliyotolewa mwishoni mwa mwaka uliopita na Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (Unesco), wakati wa maadhimisho ya Siku ya Kujua Kusoma na Kuandika, huku Tanzania ikiwa haina taarifa rasmi kuhusu idadi ya watu wasiojua kusoma wala kuandika.
Ripoti ya Unesco inasema kuwa, watu wasiojua kusoma na kuandika duniani ni milioni 774 na kwamba mwaka 2002 idadi ya mbumbumbu hapa nchini ilikuwa milioni 6.2, hali inayoonyesha kwamba idadi ya watu hao inazidi kuongezeka siku hadi siku.
Tutakuwa hatukosei iwapo tutasema hali hiyo inaipeleka nchi yetu kuzimu. Kama idadi ya mbumbumbu imepanda kutoka asilimia 6.2 hadi asilimia 33 katika kipindi cha miaka 12 tu, tutegemee kwamba miaka 15 ijayo zaidi ya nusu ya Watanzania watakuwa hawajui kusoma wala kuandika iwapo Serikali itaendelea kupuuzia suala la elimu kwa kisingizio cha ‘ufinyu wa bajeti’.
Nguvu na fedha nyingi vinaelekezwa katika masuala ya kisiasa na mambo mengine ya yasiyo na tija, kwani huko ndiko kwenye masilahi ya moja kwa moja kwa wanasiasa.
Jambo la kusikitisha ni kuwa, hata mafanikio tuliyokuwa tumeyapata katika sekta ya elimu tumeshindwa kuyatunza, kuyaendeleza na hata kuyaenzi.
Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima ilipoanzishwa kwa Sheria Namba 12 ya mwaka 1975, Sura ya 139, ilitoa matokeo makubwa katika muda mfupi, ambapo idadi ya watu wanaojua kusoma na kuandika ilipanda kwa kasi ya ajabu, huku Tanzania ikisifika duniani kwa kufanikisha elimu ya watu wazima.
Hata hivyo, kutokana na elimu hiyo kupuuzwa na serikali zilizofuata, maelfu ya watu waliokuwa tayari wamejua kusoma na kuandika walirudi kwenye umbumbumbu.
Tunachojaribu kusema hapa ni kwamba hatujawekeza vya kutosha katika elimu, hasa Elimu ya Watu Wazima. Pamoja na taasisi hiyo kuandaa na kutekeleza programu kwa ajili ya mafunzo ya walimu na viongozi wa Elimu ya Watu Wazima, bado kuna upungufu mkubwa katika kuendesha programu za waliomaliza elimu ya msingi kupitia Elimu Masafa pamoja na programu za Elimu kwa Umma, Elimu ya Watu Wazima na Elimu Isiyo Rasmi.
Kutokana na ufinyu wa bajeti programu hizo haziendeshwi kwa ufanisi uliotarajiwa. Kwa mfano, umekuwapo uhaba wa vitendea kazi na rasilimali watu, ikiwa ni pamoja na tovuti ya taasisi hiyo kuendeshwa tu kwa lugha ya Kiingereza.
Matokeo yake ni taasisi hiyo kupoteza muda katika kushughulikia mambo madogomadogo. Hivi sasa imeanza kuvifunga vituo vinavyotoa elimu ya sekondari nje ya mfumo rasmi ambavyo havijasajiliwa chini yake. Utaratibu huo pengine umelenga kuiletea mapato, lakini tunadhani ingebuni utaratibu mbadala wa kuviwezesha vituo hivyo kutoa elimu bora pasipo kuviweka katika misukosuko isiyo ya lazima.

Share this:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia

 
Back To Top
Copyright © 2014 MOUNT KILI NEWS. Designed by OddThemes | Distributed By Gooyaabi Templates