Ticker

6/recent/ticker-posts

WAFUGAJI WA KABILA LA BARBAIG WAMLALAMIKIA MWEKEZAJI



WAFUGAJI wa kabila Barbaig waishio porini katika pori lililopo eneo la Maramboi,kijiji cha Mdorii wilayani Babati mkoani Manyara,wamemlalamikia mwekezaji  wa Kifaransa anayedaiwa kumega eneo lao kibabe na kufanya makazi ya kudumu ikiwemo kujenga hotel ya kitalii bila kuwashirikisha huku akitumia walinzi wake kuwanyanyasa kwa kuwachapa viboko na kuwafungulia kesi mbalimbali polisi ili wayakimbie makazi yao.


Aidha wameeleza kuwa licha ya kupeleka malalamiko yao mara kadhaa kwenye vyombo vya dola na viongozi mbalimbali eneo hilo,wamekuwa hawasikilizwi zaidi ya kupuuzwa na baadhi yao kujikuta wakigeuziwa kibao kwa kubambikizwa kesi mbalimbali katika kituo cha polisi Minjingu.


Mwekezaji huyo aliyetajwa kwa jina la Nicholaus Negre(38) anadaiwa kuviweka mfukoni vyombo vya dola,waziri wa Mali asili na Utalii,Hamis Kagasheki pamoja na viongozi mbalimbali waliopo eneo hilo kiasi cha kushindwa kusema lolote juu yake na kumwacha aendelee kutenda atakavyo kwa wafugaji hao bila kuchukuliwa hatua za kisheria,huku akimweleza mwandishi wa habari kuwa hata habari hizi zikimfikia waziri Kagasheki hatishiki kwani ,waziri hiyo anamfahamu.


Wafugaji hao wamedai kuwa licha ya kushinda rufaa yao katika kesi ya msingi walioshitakiwa baraza la Ardhi na nyumba na mwekezaji huyo  , bado vitendo vya unyanyasaji vinavyofanywa na walinzi wa mwekezaji huyo vinaendelea na hawana pa kukimbilia baada ya viongozi mbalimbali katika wilaya ya Babati na mkoa kudaiwa kuwekwa mfukoni na Mwakezaji huyo.


Mmoja wa wafugaji hao,Assecheck Yonas(68) alisema kuwa katika eneo hilo la Maramboi lenye ukubwa wa hekari 45 walianza kuishi tangu miaka ya 1960 wakiendesha  shughuli zao  za ufugaji na uwindaji na kwamba ilipofika mwaka 2008 waliletewa hati ya wito katika  mahakama hiyo wakidaiwa kuvamia eneo hilo .


Aidha katika mwenendo huo wa kesi  wafugaji hao,wakiwakilishwa na wakili, John Materu wa kampuni ya uwakili ya Materu ya jijini Arusha,walishindwa mara mbili lakini mwaka 2012 walikata rufaa kwa majaji watatu katika mahakama kuu ya Arusha na ilipofika  tarehe 15.3.2013 hukumu ilitolewa kuwa wameshinda rufaa.


Mahakama hiyo ilijiridhisha  kuwa hapakuwa na muhtasari wa kikao cha kijiji kilichoketi na kukubaliana kulitwaa eneo hilo kwa mwekezaji,ambapo mahakama iliamuru wafugaji hao kuendelea kuishi katika eneo hilo pasipo na shaka yoyote.


Kwa upande wa mwekezaji huyo,Nicholaus akizungumza na mwandishi wa habari alisema kuwa alipatiwa eneo hilo kihalali baada ya kuomba kwa uongozi wa kijiji mwaka 2008 na kuonyeshwa eneo hilo lenye ukubwa hekari 45 .


‘’mimi nilikuja kama mwekezaji na nikaomba eneo kwa kijiji nikaonyeshwa hakari 45kwa ajili ya kujenga na kuendeleza utalii’’alisema Nicholaus


Aidha alikiri kuwakuta wafugaji hao na alipohoji uhalali wa wafugaji hao ndani ya eneo hilo alijibiwa kuwa hao ni watu wa kuondoka  na watahama muda wowote,hakuna sababu ya kuwa na mashaka na uwepo wao.


Hata hivyo alisisitiza kwa kusema kuwa haogopi kiongozi yoyote wa ngazi yoyote hapa nchini,na kueleza kuwa hata wakienda kulalamika kwa waziri wa maliasili na utalii ,Hamis Kagasheki hawatasaidiwa chochote kwani wanafahamiana vizuri na waziri huyo .


‘’mimi siogopi mbunge wala polisi ana kiongozi yoyote hata kama wataenda kwa Kagasheki hawataambilia chochote kagasheki ananifahamu vizuri’’alisisitiza Nicholaus kwa kujiamini.


Hata hivyo katika hali ya kushangaza alisema kuwa yeye  hana mgogoro na wafugaji hao ila wenye mgogoro huo ni uongozi wa kijiji hicho pamoja na Jumuiya ya hifadhi ya wanyama pori Burunge,(WMA Burunge)ambao alidai ndio wamiliki na wasimamizi wa maeneo ya hifadhi ya wanyama pori.

Jitihada za kumpata waziri Kagasheki kupitia simu yake ya kiganjani zilishindikana kwani mara zote alipokuwa akitafutwa alidai yupo kwenye kikao cha bunge dodoma.


Naye mwenyekiti wa kijiji hicho ,Erasto Belela alisema kuwa pamoja na mahakama ya rufaa kuwapa ushindi ila kijiji kina taratibu zake na kimetenga  eneo la ekari tatu kwa kila mfugaji ili ahame katika eneo hilo na kumpisha mwekezaji ,hata hivyo alikanusha suala la kuwekwa mfukoni yeye na wenzake na mwekezaji huyo.

Post a Comment

0 Comments