Ticker

6/recent/ticker-posts

MAHAKAMA YAMUAGIZA MENETA WA TRL KUREJESHA MAGARI YA MWALE

MAHAKAMA  ya hakimu mkazi Arusha, imemwagiza Meneja wa mamlaka ya mapato (TRA)mkoani Arusha ,kutekeleza amri ya mahakama kwa kukabidhi haraka magari saba ya kifahari ya wakili maarufu nchini Median Mwale inayoyashikilia.

Akitoa maamuzi hayo  hakimu mfawidhi wa mahakama hiyo,Charles Magesa alisema kuwa kitendo cha mawakili wa serikali Fredrick Manyanda na Neema Ringo kuendelea kuzuia magari hayo ambayo mahakama ilishayatolea maamuzi ni kuidharau mahakama na ni kinyume cha sheria .

Alisema kuwa  tangu kufunguliwa kwa shauri hilo la jinai lililofunguliwa agosti 9 mwaka jana,linalomkabili mshitakiwa Mwale, shauri hilo limeshindwa kuendelea kutokana na mawakili wa serikali kuendelea kuweka mapingamizi yasiyo ya msingi ya kuzuia magari ya mshitakiwa Mwalena kusababisha kutoendelea kwa kesi ya msingi  inayomkabili.

Hakimu Magesa alisisitiza kuwa kitendo cha mawakili wa serikali kupitia ofisi ya mwanasheria mkuu, kuandika barua  TRA ya kuzuia maamuzi ya mahakama ya kuitaka TRA mkoani hapa isikabidhi magari hayo ni utovu wa nidhamu na ni kinyume cha sheria  ,kwani alisema hakuna mwenye mamlaka ya kuzuia amri halali ya mahakama ispokuwa mahakama za juu pekee .

Hakimu huyo alisema awali mahakama hiyo  ilitoa hukumu Machi  7 mwaka huu yakutaka wakili Mwale arudishiwe magari hayo hata hivyo upande wa serikali haukuridhika na maamuzi hayo na kukata rufaa mahakama kuu chini ya Jaji Kakusulo Sambu.

Alisema kuwa,  mahakama  hiyo iliridhika na maamuzi ya hakimu Magesa na kutaka faili la kesi hiyo  lirudishwe katika mahakama hiyo ya hakimu mkazi kwa ajili ya kuendelea kusikilizwa shauri la msingi linalomkabili.

Hata hivyo mawakili hao wa serikali waliendelea kupiga danadana na mara nyingi wamekuwa hawafiki mahakamani na wakifika wanatoa sababu zisizo kuwa za msingi na kufanya kuahirishwa kwa shauri hilo.

Wakati huo huo;hakimu Magesa ametupitia mbali maombi ya mawakili wa serikali waliyowasilisha mahakamani hapo ya kutaka ajitoe kwenye shauri hilo ili haki iweze kutendeka wakidai kuwa ,hakimu Magesa amekuwa na ukaribu na ndugu wa mshtakiwa.

Pia alidai kuwa mawakili hao walitoa sababu nyingine kuwa ofisi ya mshitakiwa Mwale ipo jijini Arusha huku  mahakama  nayo ikiwa Arusha hivyo kutakuwa na mwingiliano kiutendaji  na kufanya haki isitendeke,kadhalika sababu  nyingine wakidai mshitakiwa ni mkazi wa Arusha  hivyo anaweza kuwa na mwingiliano naye  wa karibu ama ndugu zake.

Hakimu Magesa alisema baada ya kuzipitia hoja hizo alibaini kuwa hazina mashiko na wala haziihitaji elimu ya darasa la saba kuzielewa na kuwataka mawakili hao kurudi darasani ili kujiridhisha na elimu walio nayo ,kwani ameshangazwa na mawakili hao wasomi tena wa ngazi za juu  kuwa mbumbumbu wa kutojua vifungu vya sheria kwa kutoa hoja zisizo za msingi kama hizo.

Alisisitiza kuwa mahakama haitoi maamuzi yanayowapendeza wao bali inafuata sheria katika kutekeleza maamuzi yake ili haki iweze kutendeka ,hata hivyo alifafanua  kuwa sababu za msingi za kutaka hakimu ajitoe ni pamoja na ushahidi unaoonyesha kuwa hakimu ama jaji ana mahusiano ya kindugu yenye maslahi na wahusika wa kesi.

Aidha alisema sababu nyingine ni kuwepo kwa ushahidi unaoonyesha kuwepo kwa manufaa kwa  jaji ama hakimu kwa mshtakiwa  katika shauri la kesi husika.

Alisema kutokana na sababu hizo upande wa mashtaka umeshindwa kuthibitisha hoja zao ,hivyo hakimu Magesa alisema mawakili hao wanajaribu kupoteza muda  katika shauri hilo na kuutaka upande wa mashtaka kukamilisha upepepezi haraka ili kesi ya msingi iweze kumalizika na sio kupoteza muda kwa sababu zisizofaa.

Hata hivyo hakimu magesa aliwataka mawakili hao wa serikali kuacha kuchezea kodi za wananchi katika kesi hiyo kwa kutumia gharama kubwa kusafiri,kula  na kulala hotelini kwa kuwa wamekuwa wakichelewesha kesi hiyo kwa kuahirishwa huku wakiiambia mahakama kuwa maofisa wao wako nje ya nchi wakifuatilia nyaraka mbalimbali za kesi hiyo.

Hakimu Magesa aliahirisha shauri hilo hadi julai kumi na tatu mwaka huu litakapotajwa tena na kuwataka mawakili wa serikali kufika mahakamani hapo.

Post a Comment

0 Comments