JAMII YATAKIWA KUTAMBUA UMUHIMU WA KUWALINDA WATOTO

JAMII imetakiwa kutambua umuhimu wa kuwalinda watoto na kufahamu haki zao za msingi huku wakitambua kuwa swala la kuwalinda  watoto ni la kwetu sote badala ya kuwaachia serikali na mashirika binafsi.

Hayo yalisemwa na Mratibu wa shirika la Mkombozi la mjini Arusha, Herry Adili wakati akizungumza katika tamasha lililolenga haki za mtoto na kuwashirikisha wadau mbalimbali kutoka kwenye jamii juu ya umuhimu wa kumlinda mtoto na kumpatia haki zao za msingi.

Alisema kuwa, jamii inayowazunguka watoto hao ndio inayopaswa kuhakikisha inawalinda na matukio mbalimbali ya unyanyasaji yanayofanya kwenye jamii zao ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mtoto anapewa nafasi ya kushiriki kikamilifu badala ya kunyanyapaliwa.

Alisema kuwa,umefika wakati sasa wa jamii kuchukua hatua na kuanza kutokomeza matukio mbalimbali ya unyanyasaji  wanayofanyiwa watoto hao na kujikuta wengi wao wakiishia mitaani na hata wengine kujiunga na makundi mbalimbali yanayowapotosha.

Aliongeza kuwa,jamii inapaswa kutambua kuwa ina wajibu mkubwa sana wa kumlinda mtoto yoyote aliyeko katika jamii kwa kumpatia haki zake za msingi badala ya kutegemea mashirika mbalimbali na serikali kufanya mambo hayo.

Naye Mwelimishaji  kutoka shirika hilo la Mkombozi ,Fredrick Mbise alisema kuwa shirika hilo limeweza kufanya utafiti wa awali chini ya ofisa wa shirika hilo raia wa kigeni,Anna Spector kuhusu haki za watoto na hisia zao juu ya ulinzi,kuanzia mwezi machi  hadi mei mwaka huu,ambapo limebaini kuwa watoto hao wanaelewa haki zao.

Alisema utafiti huo  ulieleza kuwa, theluthi mbili ya watoto wanaamini kwamba wazazi au watu wazima wana uwezo wa kuondoa haki za watoto na nusu ya watoto walisema kuwa wazazi ndio wanaoamua  ni haki zipi ambazo watoto wanapaswa kuwa nazo.

Alisema kuwa, jumla ya watoto 745 walishiriki katika utafiti huo ambapo kati ya hao watoto 603 wanatokea mashuleni huku watoto 142 wapo kwenye jamii , ambapo maeneo yaliyofanyiwa utafiti huo ni  moshi mjini ,moshi vijijini na manispaa ya Arusha .

Aliongeza kuwa, watoto wengi wanahitaji haki zao za msingi kama vile kupata elimu, mavazi,malazi, chakula na ulinzi na endapo watapatiwa haki zao  itawasaidia kwa kiasi kikubwa sana kutulia na hatimaye kujidhamini wao wenyewe.

Alisema kuwa, baada ya utafiti huo wamechukua uamuzi wa kuwajulisha wadau mbalimbali katika jamii juu ya umuhimu wa kumjali mtoto na kumpatia haki zake za msingi ikiwa ni pamoja na kumlinda juu ya matukio mbalimbali ya unyanyasaji .

About Woinde Shizza

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.

0 Comments:

Post a Comment

unashauriwa kutoa maoni muda na wakati wowote na kama unahabari yeyote unaruhusiwa kututumia