Ticker

6/recent/ticker-posts

RWANDA YAKANA KUKOSA FEDHA KUGHARIMIA KESI YA UWINKINDI

Rwanda, Jumanne imekanusha ripoti kwamba timu ya utetezi ya mshitakiwa wa mauaji ya kimbari, Mchungaji Jean Uwinkindi imekosa fedha za kuwawezesha kufanya upelelezi na kuwatafuta mashahidi wa kumtetea mteja wao.
Uwinkindi ni mshitakiwa wa kwanza wa Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR) kesi yake kuhamishiwa nchini Rwanda,kusikilizwa katika mahakama ya nchi hiyo.
Gatera Gashabana,Wakili wa utetezi wa Uwinkindi alitoa malalamiko ya kukosekana kwa fedha, kwa mujibu wa msimamizi wa mwenendo wa kesi hiyo wa ICTR, Anees Ahmed. Lakini kwa upande wake, Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Rwanda, Martin Ngoga alisema Jumanne kwamba hakuna uhaba wa fedha kugharimia kesi hiyo.
‘’Serikali inajua majukumu yake ya kuwezesha upande wa utetezi chini ya mfumo wa msaada wa kisheria,’’ Ngoga aliliambia Shirika la Habari la Hirondelle kwa simu. ‘’Shughuli yoyote ya upande wa utetezi inayoruhusiwa na mahakama italipwa.Hakuna uhaba wa fedha kwa ajili hiyo.’’
‘’Kama upande wa utetezi unataka kufanya shughuli yoyote, hawana budi kuiomba mahakama,’’ Ngoga aliiambia Hirondelle. Alisema hakuna ombi la aina hiyo mbele ya jaji na kwamba ‘’hakuna haja ya kupiga kelele kwa jambo ambalo halijafikishwa mbele ya mamlaka husika.’’
Alipokuwa chini ya kizuizi cha ICTR, Mchungaji Uwinkindi kama mtu asiyekuwa na uwezo wa kujilipia huduma za kisheria, alikuwa anapewa huduma hiyo na mahakama hiyo ya Umoja wa Mataifa.Lakini Mbele ya mahakama ya Rwanda, gharama za msaada wa kisheria zinatakiwa kulipwa na serikali ya Rwanda.
Kwa mujibu wa ripoti ya msimamizi wa mwenendo wa kesi hiyo, msaada wa kisheria unaotolewa kwa Wakili Kiongozi na Msaidizi wake unagharimia huduma tu na hauruhusu kulipia gharama za kukodisha wapelelezi wa kesi au gharama za kuwatafuta mashahidi watarajiwa, kuchukua maelezo yao na kuhakikisha kuwepo mbele ya mahakama wanapohitajika.
ICTR iliamuru kuhamishwa kwa kesi ya Uwinkindi kwenda kusikilizwa nchini Rwanda Juni mwaka jana na Mahakama ya Rufaa ilithibitisha uamuzi huo Desemba, 2011. Uwinkindi alihamishiwa nchini Rwanda Aprili 19, 2012.
Wafanyakazi wawili wa ICTR waliteuliwa kuwa wasimamizi wa muda wa mwenendo wa kesi hadi hapo makubaliano yatakapokamilishwa ya kupata wasimamizi kutoka Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu(ACHPR).
Mchungaji Uwinkindi anashitakiwa kwa mauaji ya kimbari na kuteketeza kizazi. Kwa mujibu wa Msimamizi wa ICTR, upande wa mwendesha mashitaka uko tayari kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo.

Post a Comment

0 Comments